• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 11:33 PM
Liverpool yafufuka

Liverpool yafufuka

Na MASHIRIKA

LIVERPOOL walitandika Newcastle United 2-0 ugani St James’ Park mnamo Jumamosi na kuweka wazi azma yao na kuwa miongoni mwa vikosi vinne vya kwanza kwenye jedwali la Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) msimu huu.

Miamba hao walishuka dimbani wakiwa na kiu ya kuendeleza matokeo bora baada ya kupepeta Everton 2-0 mwanzoni mwa wiki iliyopita. Ushindi dhidi ya Everton ugani Anfield ulikuwa wao wa kwanza mwaka huu.

Miamba hao walipata magoli yao dhidi ya Newcastle kupitia kwa Darwin Nunez na Cody Gakpo aliyeshirikiana vilivyo na Mohamed Salah na kufungia Liverpool katika pambano la pili mfululizo.

Newcastle walikamilisha mechi hiyo na wachezaji 10 pekee uwanjani baada ya kipa Nick Pope kuonyeshwa kadi nyekundu kwa kosa la kumchezea Salah visivyo. Mlinda-lango huyo raia wa Uingereza atakosa sasa fainali ya Carabao Cup itakayokutanisha waajiri wake na Manchester United ugani Wembley mnamo Februari 26, 2023.

Martin Dubravka aliyejaza nafasi ya Pope dhidi ya Newcastle, hatanogesha fainali ya Carabao Cup msimu huu kwa kuwa aliwahi kuwajibikia Man-United katika hatua za kwanza za kipute hicho muhula ulipoanza.

Hali hiyo kunaacha Newcastle katika ulazima wa kutegemea maarifa ya kipa wa zamani wa Liverpool, Loris Karius, dhidi ya Man-United kadri wanavyofukuzia taji la kwanza tangu 1969 walipojizolea ubingwa wa Inter-Cities Fairs Cup.

Newcastle sasa wamepoteza mechi mbili pekee ligini muhula huu na kichapo chao cha kwanza kilikuwa dhidi ya Liverpool waliowapepeta 2-1 mnamo Agosti 2022 ugani Anfield.

Ushindi wa Liverpool ulikuwa kitulizo kikubwa kwa kocha Jurgen Klopp aliyeshuhudia masogora wake awali wakipoteza ugenini dhidi ya Brentford (3-1), Brighton (3-0) and Wolverhampton Wanderers (3-0). Sasa wana alama 35 kutokana na mechi 22 na pengo la pointi sita pekee ndilo linawatenganisha na Newcastle ambao wametandaza mchuano mmoja zaidi.

MATOKEO YA EPL (Jumamosi):

Aston Villa 2-4 Arsenal

Brentford 1-1 Palace

Brighton 0-1 Fulham

Chelsea 0-1 Southampton

Everton 1-0 Leeds

Nottm Forest 1-1 Man-City

Wolves 0-1 Bournemouth

Newcastle 0-2 Liverpool

TAFISIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Hoki: Butali 3-bora Klabu Bingwa Afrika

Jinsi Man-City walivyopoteza nafasi ya kurejea kileleni mwa...

T L