• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 9:35 PM
Maafande wa Kenya Police wazima MSC

Maafande wa Kenya Police wazima MSC

Na JOHN KIMWERE

WAFALME wa zamani katika mpira wa magongo, Kenya Police walikung’uta Mombasa Sports Club (MSC) mabao 3-0 kwenye mechi ya Ligi Kuu iliyopigiwa City Park, Nairobi. Maafande hao walionyesha mchezo mzuri na kuhakikisha wamelipiza kisasi baada ya kunyukwa na Western Jaguars wiki iliyopita.

Chini ya nahodha, Victor Wekesa walipata bao la kwanza dakika ya nne kupitia Robert Masibo. Masibo aliongezea bao la pili na tatu dakika ya 45 na 60. ”Tulitumia mtindo tofauti maana wachezaji wa safu ya kiungo ndio waliokuwa wanafunga baada ya wenzao wa safu ya mbele kupata upinzani mkali,” kocha wa Police, Patrick Mugambi alisema na kushukuru wachezaji wake kwa ushindi huo. Naye nahodha, Victor Wekesa alishukuru wenzake na kuwataka wachangamke kuonyesha uwezo wao.

Mjini Kakamega, kwa mara ya pili wenyeji Western Jaguars waliangukia pua kwa kuzabwa bao 1-0 na Wazalendo. Jaguars ilikubali kipigo hicho siku moja baada ya kulala kwa bao 1-0 mbele ya Mashujaa ya Chuo Kikuu cha Kimataifa cha USIU-A.

Kwenye matokeo za mechi hizo kitengo cha kina dada, malkia wa mchezo huo Blazers walizaba DFG Wolverines mabao 1-0 ugani City Park, Nairobi Bao hilo lilitupiwa kimiani na Carol Gushu. Mjini Kisumu, Florence Karanja alicheka na wavu mara moja na kubeba Spartans ya Chuo Kikuu cha Kimataifa cha USIU-A kuzaba Lakers bao 1-0.

”Ninashukuru wachezaji wangu kwa kukabili vilivyo wapinzani wao na kuzoa alama zote tatu,” kocha wa USIU-A, Willis Okeyo alisema na kuongeza kuwa wamepania kuendeleza mtindo huo. Kwenye mechi za Supa Ligi ya wanawake, wasomi wa Chuo Kikuu cha Kenyatta (KU) walibeba ufanisi wa bao 1-0 dhidi ya Mombasa Sports Club (MSC). Nayo Nairobi Chapel Ladies ilidungwa bao 1-0 na Multimedia University (MMU).

You can share this post!

Brentford yazamisha chombo cha West Ham United ligini

Wafanyakazi wa kampuni ya KPLC washtakiwa kwa wizi

T L