• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 7:55 AM
Mourinho pabaya Italia baada ya Roma kuzamishwa tena ligini

Mourinho pabaya Italia baada ya Roma kuzamishwa tena ligini

Na MASHIRIKA

MASAIBU ya kocha Jose Mourinho katika kampeni za Ligi Kuu ya Italia (Serie A) msimu huu yaliendelezwa na mabingwa watetezi Inter Milan waliopepeta waajiri wake AS Roma 3-0 mnamo Jumamosi ugani Olimpico.

Roma walikosa huduma za fowadi Tammy Abraham katika mchuano huo ulioshuhudia Inter wakipaa hadi nafasi ya pili jedwalini kwa alama 37, moja pekee nyuma ya viongozi AC Milan waliokung’uta limbukeni Salernitana 2-0.Roma wanakamata nafasi ya tano kwa alama 25 baada ya kupoteza mechi ya saba kutokana na 15 zilizopita.

Ni pengo la alama tisa linalowatenganisha sasa na nambari nne Atalanta waliocharaza Napoli 3-2.Matokeo ya Roma dhidi ya Inter yalishuhudia Mourinho akifikia rekodi yake ya awali ya kupoteza mechi ya nyumbani kwa idadi kubwa zaidi ya mabao.

Kilichokuwa kikosi chake cha Manchester United kiliwahi kupigwa 3-0 na Tottenham Hotspur ligini EPL mnamo Agosti 27, 2018. ugani Old Trafford.Roma kwa sasa wamepoteza idadi kubwa zaidi ya mechi za Serie A (16) katika mwaka mmoja kwa mara ya kwanza tangu 1950 walipopigwa mara 20.

Kwingineko, rekodi ya kutoshindwa kwa kocha Xavi Hernandez kambini mwa Barcelona ilipigwa breki kali na Real Betis waliopokeza miamba hao wa Ligi Kuu ya Uhispania (La Liga) kichapo cha 1-0 mnamo Jumamosi ugani Camp Nou.

Xavi aliongoza waajiri wake kumenyana na Betis baada ya kushinda mechi mbili ligini pamoja na kuambulia sare tasa dhidi ya Benfica kwenye Klabu Bingwa Ulaya (UEFA).?Kichapo kutoka kwa Betis sasa unawaweka Barcelona katika nafasi ya saba jedwalini kwa alama 23, sita nyuma ya mabingwa watetezi Atletico Madrid wanaofunga orodha ya nne-bora baada ya kupigwa 2-1 na Mallorca katika uga wa nyumbani.

Real Madrid ya kocha Carlo Ancelotti ilifungua mwanya wa alama nane kileleni mwa jedwali la La Liga baada ya kuchapa Real Sociedad 2-0. Kikosi hicho cha kocha Carlo Ancelotti sasa kimejizolea alama 39 na kinajiandaa kuvaana na Atletico katika mechi ijayo ligini.

Ilikuwa mechi ya pili mfululizo kwa Sociedad inayoshikilia nafasi ya tano kwa pointi 29 kupoteza baada ya kujivunia rekodi ya kutoshindwa katika michuano 13 ya La Liga.?Katika Ligi Kuu ya Ujerumani (Bundesliga), fowadi Robert Lewandowski alipachika wavuni mabao mawili na kusaidia waajiri wake Bayern Munich kusajili ushindi wa 3-2 dhidi ya Borussia Dortmund ugani Signal Iduna Park.

Ushindi huo uliwezesha Bayern kufungua pengo la alama nne kileleni mwa jedwali na sasa mabingwa hao watetezi wanajivunia alama 34 kutokana na mechi 14 zilizopita.?Lewandowski sasa ana magoli 66 kutokana na mechi 55 za mwaka huu wa 2021 na amecheka na nyavu za wapinzani mara 118 kutokana na mechi za ugenini kwenye Bundesliga.

You can share this post!

JAMVI: Mlima utatoa nani mgombea mwenza wa Raila 2022?

Arsenal kwenye mizani

T L