• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 8:55 PM
Mwanasoka anayelenga kufuata nyayo za Sergio Ramos wa PSG

Mwanasoka anayelenga kufuata nyayo za Sergio Ramos wa PSG

Na PATRIC KILAVUKA

Ni difenda wa kutamba uwanjani akilenga ustadi wa soka wa mlinda ngome Sergio Ramos wa PSG.

Alex Ngunjiri,16,anasema ufundi wa uchezaji wa mchezaji huyo unamfaa kutokana na pasi zake ndefu na za uhakiki na anavyodhibiti boli. Huvitilia maana vigezo alivyovitaja vya mwanakabumbu Ramos wakati wa mchezo na anaimarika kila uchao.

Mwanasoka Ngunjiri ni mwanafunzi wa kidato cha tatu Shule ya Upili ya Kabete,kaunti ndogo la Kabete. Hata hivyo, elimu ya msingi aliipata Shule ya Msingi ya Eneza Premier, Wangige, kaunti ndogo ya Kabete. Yeye ni mtoto wa tatu miongoni mwa watoto wanne wa Peter Ngunjiri Muthee na Bi Anne Ngunjiri.

Akiwa shule ya sekondari, aliweza kucheza hadi kiwango cha Kaunti japo shule yake ilikomolewa na Shule ya Wavulana ya Alliance, 2019 kabla msambao wa corona. Mwanakandanda huyu amelelewa kitalanta na timu ya U -17 ya Tebeka Sports Academy kabla kupandishwa ngazi katika timu ya Kabete Olympic ambayo iliundwa mwishomwisho mwa mwaka jana kukuza vipawa na kuandaa jukwaa ambalo vijana watapewa fursa ya kujitanua kisoka.

Chini ya Kocha mkuu Sammy Muniu na mkufunzi Brian Omuyaku Bertlet, amejiongezea nchi ya ujuzi kupita mawaidha yao ya kuimarisha nguzo za talanta yake pamoja na mazoezi makali ambayo anapiga kila Jumatatu hadi Ijumaa uwanjani Kiingero. Mbali na kuchezea vipute wikendi.

Mwanasoka Alex Ngunjiri akidhibiti boli wakati wa mechi yao timu ya Kabete Olympic dhidi ya Barcelona ugani Approved, Lower Kabete…Picha/PATRICK KILAVUKA

Yeye si difenda tu ila, humpata mshawashi wa kufuma magoli kwa kucheza kama mwanasoka wa pembeni wa kutamba hali ambayo humpelekea kucheka na nyavu. Katika mashindano ya shule za upili, alifunga magoli matatu kufikia kiwango cha Kaunti.

Katika kipute cha Wamachuru Cup, 2022 ambacho kinaendela kuwaka moto, tayari amepachika mabao matatu. Anasema ndugu yake David Simiyu amekuwa akivutio chake cha uchezaji katika ukoo wao.Katika kujiweka fiti kuimarisha afya yake, ameepukana na matumizi ya mihadarati yoyote kwani anasema maono yake ni kucheza soka hadi upeo wa juu majaliwa ya Maulana.

Anaazimia kujituma angalau avae jezi la AFC Leopards au timu ya Harambee Stars. Hata hivyo,ughaibuni yeye hushabiki Manchester United. Changamoto yake ni kwamba, wakati mwengine hubanwa na masomo na kukosa wakati mwafaka wa kujinoa, japo hufanya mazoezi mepesi ya kibinafsi. Pia,vifaa vya mazoezi vya kujikuzia pia huwa kisiki kwani yeye bado mwanafunzi.

Angependa kuwashukuru wazazi na makocha kwa sapoti yao ya hali na mali na mawaidha umbali amefika. Pasi na kuacha nyuma mashabiki ambao humtia motisha ya kuona matunda ya jasho lake la kujituma katika ulingo wa kabumbu inadhihirika.

Mwanasoka Alex Ngunjiri akipongezwa na kocha Brian Omuyaku Bertlet baada ya mchuano wao dhidi ya Barcelona ugani Approved,Lower Kabete…Picha/PATRICK KILAVUKA

You can share this post!

Mdalasini na faida zake mwilini

Mshukiwa mkuu katika kashfa ya NYS kukamatwa

T L