Na GEOFFREY ANENE
MKENYA Seline Ahoya akishirikiana na raia wa Misri Jina Elmashad walipoteza katika fainali ya mashindano ya Afrika ya tenisi ya wachezaji wasiozidi umri wa miaka 14 mjini Antananarivo, Madagascar, jana Jumamosi.
Dakika chache baada ya kubanduliwa na Mmisri Habiba Essam Habib katika nusu-fainali ya mechi ya mchezaji mmoja kila upande kwa kupigwa 6-1, 6-0, Ahoya, na Elmashad, walipoteza dhidi ya Habib na Dareen Hosam 6-1, 6-3 katika fainali ya wachezaji wawili kila upande.
Kufika nusu-fainali ya mchezaji mmoja kila upande, bingwa wa Afrika Mashariki U12 na U14 Ahoya aliwacharaza Soa Andriamaniraka 6-1, 6-0 na Miranda Ranaivosoa 6-1, 7-6(2) kutoka Madagascar katika raundi ya 16-bora na robo-fainali mtawalia.
Ahoya ni Mkenya pekee katika mashindano hayo ya kwanza nchini Madagascar yatakayofika kilele hapo Septemba 18. Yameleta pamoja wachezaji kutoka mataifa ya Kenya, Zimbabwe, Misri, Madagascar na Msumbiji. Mashindano ya pili yatafanyika Septemba 19-22.