Na MASHIRIKA
WEST Ham United walitoka nyuma na kulazimishia Newcastle United sare ya 1-1 katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) ugani St James’ Park.
Sean Longstaff aliyefunga mabao mawili dhidi ya Southampton mnamo Januari 31, 2023 na kusaidia Newcastle kufuzu kwa fainali ya Carabao Cup alishirikiana vilivyo na Callum Wilson aliyeweka waajiri wake kifua mbele katika dakika ya tatu.
Fabian Schar nusura afanye mambo kuwa 2-0 katika dakika ya 10 kabla ya West Ham kusawazishiwa na Lucas Paqueta kunako dakika ya 32. Bao hilo lilikuwa la kwanza kwa Newcastle kufungwa ligini tangu Novemba 6, 2022. Kikosi hicho cha kocha Eddie Howe sasa kimeambulia sare mara nne kutokana na mechi tano zilizopita za EPL.
Licha ya kujituma vilivyo katika vipindi vyote viwili vya mchezo, Newcastle walikosa kufunga bao la ushindi katika mechi hiyo iliyokuwa ya kwanza kwa fowadi Allan Saint-Maximin kunogesha ligini tangu Agosti 28, 2022.
Matokeo hayo yaliteremsha Newcastle hadi nafasi ya nne jedwalini kwa alama 40, mbili nyuma ya nambari tatu Manchester United waliokomoa Crystal Palace 2-1 ugani Old Trafford licha ya kiungo mkabaji Carlos Casemiro kuonyeshwa kadi nyekundu katika kipindi cha pili.
Ni pengo la alama nne ndilo linatamalaki kati ya Newcastle na nambari tano Tottenham Hotspur watakaokuwa wenyeji wa mabingwa watetezi Manchester City mnamo Februari 5, 2023. Man-City wanashikilia nafasi ya pili jedwalini kwa alama 45 huku West Ham wakisalia katika nafasi ya 16 kwa pointi 19 baada ya mechi 21.
MATOKEO YA EPL (Jumamosi):
Everton 1-0 Arsenal
Aston Villa 2-4 Leicester
Brentford 3-0 Southampton
Brighton 1-0 Bournemouth
Man-United 2-1 Crystal Palace
Wolves 3-0 Liverpool
Newcastle 1-1 West Ham
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO