• Nairobi
  • Last Updated May 20th, 2024 5:55 AM
Okutoyi asalimu amri robo-fainali ya wachezaji wawili wawili Monastir

Okutoyi asalimu amri robo-fainali ya wachezaji wawili wawili Monastir

Na GEOFFREY ANENE

MKENYA Angella Okutoyi na mchezaji mwenza Akanksha Nitture wamebanduliwa katika robo-fainali ya shindano la tenisi la kinadada la W15 Monastir nchini Tunisia, Alhamisi.

Wamepigana kufa-kupona, lakini wakapoteza kwa seti 2-1 za 6-7(1), 6-1, 10-4 dhidi ya Nina Radovanovic (Ufaransa) na Xinxin Yao (Uchina) ambao wanaorodheshwa wa pili katika mashindano haya.

“Tuliwasukuma vilivyo wapinzani wetu wanaoorodheshwa juu sana katika mashindano haya katika nafasi ya pili. Tulicheza vizuri, hasa kati seti ya pili ambapo tulipunguza makosa na tukaonyesha ujasiri,” alisema Okutoyi baada ya mechi hiyo waliyopoteza kwa saa moja na dakika 38.

Okutoyi na Nitture, ambaye ni raia wa India, walijikatia tiketi ya kushiriki robo-fainali baada ya kuwamwaga Zuzanna (Poland) na Magdalena Stoilkovska (North Macedonia) kwa seti 2-1 za 6-3, 1-6, 10-5 katika mchuano uliodumu saa moja na dakika 21. Radovanovic na Yao walilima Ferdaous Bahri (Tunisia) na Margaux Komano (Ufaransa) 6-2, 6-3.

Okutoyi, ambaye aliandikisha historia kwa kunyakua taji la chipukizi la Wimbledon mwezi Julai, alibanduliwa na Shrivalli Bhamidipaty kutoka India katika raundi ya kwanza ya kitengo cha mchezaji mmoja kila upande mnamo Agosti 2.

Bingwa huyo wa Kenya Open 2018 na Afrika kwa wachezaji wasiozidi umri wa miaka 18 mwaka 2021 alitoa Bhamidipaty kijasho kabla ya kusalimu amri kwa seti mbili kavu za 7-6(5), 7-5 katika klabu ya tenisi ya Monastir. Sasa, anaelekeza macho yake kwa shindano la tatu la W15 Monastir linhaloanza Agosti 15.

You can share this post!

Team Kenya ya Davis Cup tayari kwa Kombe la Afrika tenisi

TAHARIRI: Sote tuwe washindi katika kura juma lijalo

T L