NA MASHIRIKA
MANCHESTER, Uingereza
KOCHA Pep Guardiola alijitaja kama ‘mchawi’ na kumiminia sifa vijana wake wa Manchester City baada ya kuzoa ushindi wa nne mfululizo walipopiga Chelsea 1-0 ugani Stamford Bridge.
Mabingwa hao watetezi walilenga kurejea ulingoni kwa kishindo baada ya kuambulia pointi moja katika sare ya 1-1 dhidi ya Everton Januari 1.
City walijikokota katika kipindi cha kwanza ambacho wenyeji Chelsea waligonga mlingoti kupitia kwa Carney Chukwuemeka.
Guardiola alifanya mabadiliko kadhaa baada ya mapumziko yaliyoleta uhai katika timu yake katika kipindi cha pili.
Dakika tatu baada ya viungo washambulizi Riyad Mahrez na Jack Grealish kutupwa uwanjani, walishirikiana katika kupatikana kwa bao muhimu dakika ya 63.
Grealish alichanja krosi murwa iliyokamilishwa kwa ustadi na Mahrez.
Chelsea ya kocha Graham Potter ilishindwa kusawazisha, huku City ikitia kapuni alama tatu na kukata uongozi wa Arsenal hadi pointi tano.
Beki John Stones alikuwa mchezaji bora wa City kwa kukata mashambulizi kadhaa ya Chelsea.
“Hatukucheza vyema katika kipindi cha kwanza. Nashukuru Joao Cancelo kwa juhudi zake licha ya kuwa nilimchezesha katika nafasi isiyo yake,” alisema Guardiola aliyejitaja kama ‘mchawi’ baada ya mabadiliko aliyofanya kuzalisha matunda.
“Tuliimarika sana katika kipindi cha pili katika idara zote. Ushindi huu ni mkubwa sana kwetu. Riyad Mahrez, John Stones, Jack Grealish walicheza vizuri sana,” alisema Guardiola.
“Pointi hizi tatu ni muhimu sana. Wachezaji hawajasahau kuwa kwa muda mrefu tulikaa juu ya jedwali. Tuna mechi za mashindano ya Kombe la FA na Carabao kabla ya kuelekea uwanjani Old Trafford kuvaana na Manchester United ligini. Ilikuwa muhimu kupata ushindi. Tutaelekea Old Trafford halafu Spurs,’ alisema Guardiola. Wanabunduki wa Arsenal wanaongoza ligi kwa alama 44, tano mbele ya City. Chelsea inapatikana katika nafasi ya 10 kwa pointi 25.
Subscribe our newsletter to stay updated