• Nairobi
  • Last Updated May 8th, 2024 7:55 PM
Red Devils wafufuka Spurs na Arsenal wakila marungu

Red Devils wafufuka Spurs na Arsenal wakila marungu

NA MASHIRIKA

KUJIKWAA kwa Tottenham Hotspur na kuteleza zaidi kwa Arsenal katika mechi zao za Jumamosi, kulifufua matumaini ya Manchester United kukamilisha Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) ndani ya nne-bora msimu huu.

Cristiano Ronaldo aliwabeba waajiri wake mabegani akifungia Man-United mabao yote matatu – hattrick – katika ushindi wa 3-2 dhidi ya Norwich City wanaovuta mkia kwa alama 21.

Ronaldo, 37, sasa anajivunia mabao 15 katika EPL msimu huu; sawa na Diogo Jota wa Liverpool ambaye pia anasoma migongo ya Son Hueng-min (17) na Mohamed Salah (20).

Aidha, sasa ametinga jumla ya hattrick 60 katika taaluma yake ya soka.

Ufanisi huo ulikuwa mtamu zaidi kwani alijizolea jumla ya Sh127,000,000 milioni kama bonasi ya kufungia Red Devils mabao zaidi ya 20 msimu huu; Sh112,128,000 milioni kwa mabao 20 na Sh14,950,400 milioni kwa bao la ziada.

Senti hizo za pili (Sh14,950,400 milioni) zitatumwa katika akaunti yake kwa kila goli atakalofunga kuanzia sasa hadi mwisho wa msimu.

Baada ya mechi 32, Man-United sasa wanajivunia alama 54, sawa na Arsenal wana mechi moja ya akiba baada ya kutandaza michuano 31.

Mabingwa hao mara 20 wa EPL watakuwa wageni wa Liverpool hapo kesho, siku moja kabla ya Arsenal kuendea Chelsea ugani Stamford Bridge.

Huku Arsenal wakipepetwa 1-0 na Southampton uwanjani St Mary’s, Spurs pia walipokezwa kichapo sawa na hicho kutoka kwa Brighton.

Spurs, ambao pia wamecheza mechi 32, sasa wanakamata nafasi ya nne jedwalini kwa alama 57.

Mbali na kibarua kizito cha kuangusha Chelsea, Arsenal watahitaji miujiza kuzamisha Man-United, West Ham, Spurs na Everton katika mechi nne kati ya saba zilizosalia msimu huu, ili kufuzu Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) tangu 2016-17.

Kocha Mikel Arteta amekiri kwamba kudorora kwa fomu ya Gunners “kunazua hofu”; ikizingatiwa kwamba mechi dhidi ya Southampton ilikuwa ya tatu mfululizo kwa vijana wake kupoteza.

“Tumepoteza mechi kwa njia tofauti, lakini tulivyofanya dhidi ya Southampton kunatia hofu na ni vigumu kueleza,” akasema Arteta.

  • Tags

You can share this post!

Mivutano Azimio inavyohujumu mipango ya Raila kuingia Ikulu

Ragwa ahama UDA, kuwa mwaniaji huru kwa useneta

T L