Na GEOFFREY ANENE
Timu za taifa za raga ya wachezaji saba kila upande za Kenya Shujaa (wanaume) na Lionesses (wanawake) zinatarajiwa kufahamu makundi yao ya Olimpiki 2020 juma hili.
Hii ni baada ya wanaume wa Ireland na kinadada wa Ufaransa na Urusi kunyakua tiketi katika mashindano ya mwisho ya kufuzu kushiriki Olimpiki mjini Monaco mnamo Juni 20.Ireland ilichapa Ufaransa 28-19 katika fainali ya mchujo wa mataifa 12 mjini Monaco na kuungana na Shujaa, Fiji, Amerika, New Zealand, Afrika Kusini, Argentina, Canada, Uingereza, Australia, Korea Kusini na Japan kwenye Olimpiki.
“Ireland wanacheza vizuri sana. Mchezo wao ni wa kasi ya juu. Wacha tusubiri kuona watakavyocheza Olimpiki,” alisema kocha mkuu wa Shujaa, Innocent “Namcos” Simiyu mnamo Juni 21 akifichua kuwa vijana wake wataingia kambini Juni 27.
Wamekuwa mapumzikoni tangu Juni 18 baada ya Kenya kujiondoa kushiriki mashindano ya mwaliko ya Quest For 7s mjini Los Angeles, Amerika yatakayofanyika Juni 25-26.Ufaransa ililemea Hong Kong 51-0 nayo Urusi ikapepeta Kazakhstan 38-0 katika fainali mbili za kinadada na kunyakua tiketi.
Zinaungana na Kenya Lionesses pamoja na Japan, New Zealand, Amerika, Canada, Australia, Brazil, Uingereza, Fiji na Uchina kwenye Olimpiki zitakazofanyika Julai 23 hadi Agosti 8 mjini Tokyo.Mashindano ya raga ya wachezaji saba kila upande kwenye Olimpiki yatafanyika Julai 26-31.