Na JOHN KIMWERE
TIMU ya wanaume ya Trailblazers na Halmashauri ya Bandari ya Kenya (KPA) kila moja ilitia kapuni alama muhimu kwenye mechi za voliboli ya ligi kuu ziliyochezewa uwanja wa Nyayo , Nairobi.
Trailblazers ya mkufunzi, Geoffrey Omondi ilizaba Kenya Army seti 3-0 nao wanaume wa KPA walivuna seti 3-0 dhidi ya Prisons Nairobi. Trailblazers inayoshiriki kipute hicho kwa mara ya kwanza ilionyesha mchezo safi lakini kiasi ilipata ushindani mkali.
Wachezaji hao walizoa alama za 25-23, 26-24, 25-19. ”Bila shaka ninashukuru wachezaji wangu wanazidi kujiongezea tumaini la kujikatia tiketi ya kushiriki fainali za muhula huu licha ya kupoteza mchezo mmoja dhidi ya KPA,” kocha wa Trailblazers alisema na kuongeza kuwa watajaribu kurekebisha makosa yao kwenye mechi zijazo.
Nayo KPA ya kocha, Sammy Mulinge iliendelea kupiga hatua iliposajili ushindi wa pili kwa alama za 25-21, 25-13, 25-10. Mkufunzi huyo alipongeza vijana wake kwa kazi nzuri waliofanya kwenye mechi walioshiriki na kuzoa alama tano.
”Tumepania kujituma kiume tuhakikishe tumefuzu kushiriki fainali za msimu huu,” akasema na kuongeza kuwa walikuwa wanatumia mechi hizo kujiandalia kipute cha Klabu Bingwa Afrika (CAVB) mapema mwezi ujao.
Kwenye matokeo mengine, Jeshi la Ulinzi (KDF) ilipiga Prisons Kenya seti 3-1 (25-23, 15-25, 17-25, 25-21, 15-09). Nayo Administration Police (AP Kenya) ilipoteza mechi ya tatu mfululizo ilipozimwa kwa seti 3-1 (20-25, 25-22, 25-20, 25-18) na Prisons Mombasa.