• Nairobi
  • Last Updated May 12th, 2024 6:50 AM
Valencia wamtimua kocha Javi Gracia baada ya matokeo duni ligini

Valencia wamtimua kocha Javi Gracia baada ya matokeo duni ligini

Na MASHIRIKA

VALENCIA wamemfuta kazi kocha Javi Gracia baada ya miezi 10 pekee akidhibiti mikoba ya kikosi hicho.

Kutimuliwa kwa Gracia kulichochewa na msururu wa matokeo duni ambayo klabu hiyo ya Ligi Kuu ya Uhispania (La Liga) imesajili katika kampeni za msimu huu.

Katika mchuano wao uliopita, kikosi hicho kilipokezwa kichapo cha 3-2 kutoka kwa Barcelona ambao kwa sasa wanakamata nafasi ya tatu kwa alama 74, sawa na mabingwa watetezi Real Madrid. Atletico Madrid wanadhibiti kilele cha jedwali kwa pointi 76.

Kichapo kutoka kwa Barcelona kilishuhudia Valencia ikishuka hadi nafasi ya 14 jedwalini kwa alama 36, sita pekee mbele ya Huesca na Elche ambao kwa pamoja na Eibar, wako katika hatari ya kuteremshwa ngazi mwishoni mwa msimu huu. Zimesalia mechi nne pekee kwa kampeni za La Liga msimu huu kutamatika rasmi.

Gracia ambaye ni mkufunzi wa zamani wa Watford, anaondoka kambini mwa Valencia baada ya kuongoza kikosi hicho kusajili ushindi katika michuano minane pekee kati ya 34 iliyopita ligini.

“Valencia ingependa kumshukuru Gracia kwa kazi aliyotufanyia kwa kujitolea katika kipindi hicho ambapo amekuwa akidhibiti mikoba ya Valencia. Tunamtakia kila la heri katika mustakabali wake kitaaluma,” ikasema sehemu ya taarifa ya Valencia ambao ni mabingwa mara sita wa La Liga.

Aliyekuwa msaidizi wa Gracia, Salvador Gonzalez ‘Voro’ atasimamia mechi zote zilizosalia muhula huu.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Wanahabari 51 walishambuliwa wakiwa kazini – ripoti...

Jaji Mkuu afaa kuteuliwa apokezwe mikoba ndipo mtangulizi...