• Nairobi
  • Last Updated May 6th, 2024 7:55 PM
Chama cha UGM chataka Uhuru atimuliwe kwa kukiuka katiba

Chama cha UGM chataka Uhuru atimuliwe kwa kukiuka katiba

NA WACHIRA MWANGI

KATIBU Mkuu wa chama cha United Green Movement Party (UGM) Hamissa Maalim Zaja sasa analitaka bunge lipitishe hoja ya kutokuwa na imani na uongozi wa Rais Uhuru Kenyatta, baada ya korti kuamua kuwa mswada wa Mpango wa Maridhiano (BBI) ulikumbatiwa kinyume cha sheria.

Bi Zaja alisema serikali ya umoja wa nchi inafaa iundwe akisema jopo la majaji watano walioamua kesi hiyo walianika wazi kwamba Rais Kenyatta alikiuka katiba kwa kuanzisha mchakato wa BBI.

Mwanasiasa huyo alisema Rais Kenyatta aliapa kuilinda katiba na anafaa kuondoka mamlakani kwa kuidhalilisha na kutekeleza mambo kinyume na matakwa yake.

Alitoa wito kwa wabunge waanze mchakato wa kumtimua Rais mara moja ili kuitendea raia haki.

“Bunge linafaa kutekeleza wajibu wake wa kuhakikisha afisi ya Rais haikiuki katiba. Huu ndio wakati wa kumuadhibu Rais Kenyatta ambaye anawadhulumu Wakenya na kufanya mambo bila kufuata katiba,” akasema Bi Zaja.

“Mahakama kuu ilisema Rais alikiuka katiba. Bila bunge kumtimua kutoka kwa wadhifa wake, ataendelea kupuuza maamuzi ya korti na kutumia mamlaka yake vibaya,” akaongeza.

Mwanasiasa huyo alisema BBI haikuwa na umaarufu wowote nchini na wanasiasa wakuu nchini akiwemo Rais Kenyatta ndio walikuwa wakiilazimisha raia waikumbatie.Alidai kuwa hata mabunge ya kaunti, kitaifa na seneti yalipitisha ripoti hiyo kwa hofu japo walifahamu kuwa haina manufaa yoyote ya kuchangia ukuuaji wa uchumi wa nchi.

You can share this post!

Jumbe za msamaha, hisani zatawala Idd

Wakenya wafurahia Mahakama Kuu kuzima densi ya Reggae