• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 12:09 PM
JAMVI: Uhuru afanikiwa kupunguza makali ya vinara wa upinzani kwa utawala wake

JAMVI: Uhuru afanikiwa kupunguza makali ya vinara wa upinzani kwa utawala wake

Na BENSON MATHEKA

RAIS Uhuru Kenyatta hatimaye amefaulu kudhoofisha upinzani dhidi ya serikali yake kwa kumshawishi kiongozi wa ODM Raila Odinga kuunga ajenda zake.

Wadadisi wanasema, japo viongozi hao wawili walisema nia yao ni kuunganisha Wakenya,  Rais Kenyatta ndiye mshindi kwa sababu hatakuwa na upinzani wenye nguvu wa kukosoa serikali yake.”

Jubilee ilijaribu kusambaratisha upinzani kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka jana lakini ikashindwa. Kwa kukutana na Bw Odinga na kufikia muafaka, Rais Uhuru amefaulu kulemaza upinzani,” asema Bw Godfrey Aliwa, mdadisi wa masuala ya siasa na wakili jijini Nairobi.

Anaeleza kuwa waliopanga mazungumzo hayo walielewa kuwa upinzani bila Raila ni butu. “Raila ndiye nguzo ya upinzani Kenya na kwa kumleta karibu na serikali ni kusambaratisha upinzani.

Lengo hapa ni kuhakikisha Rais Kenyatta hatakuwa na upinzani wenye nguvu kumsumbua katika kipindi chake cha pili na cha mwisho uongozini,” alisema Bw Aliwa.

Mbali na upinzani kuwa na wabunge wachache, wengi wao ni wa chama cha ODM cha Bw Raila ambao tayari wameanza kuchangamkia muafaka wake na Rais Kenyatta.

Washirika wa Bw Raila katika NASA, Kalonzo Musyoka wa Wiper Democratic Movement, Moses Wetang’ula wa Ford-Kenya na Musalia Mudavadi wa Amani National Congress hawakuhusishwa katika muafaka huo.

Baadhi ya washirika wa kisiasa wa Bw Musyoka, Bw Wetangula na Bw Mudavadi wamenukuliwa wakitaka chama cha ODM kuondoka NASA ili wachukue nafasi ya upinzani rasmi. Hata hivyo, kulingana na Bw Aliwa, hata kama wangeachiwa NASA, hawataweza kukosoa serikali alivyokuwa akifanya Bw Raila.

“Aliyenufaika pakubwa ni Rais Kenyatta kwa sababu atakuwa na mteremko kwa kukosa upinzani thabiti katika kipindi chake cha mwisho mbali na Raila kumtambua kama rais,” alisema.

Chini ya Bw Raila na wanasiasa wake wa ODM, upinzani uliongoza maandamano yaliyong’oa makamishna wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) chini ya aliyekuwa mwenyekiti Isaack Hassan.

Ni Bw Odinga ambaye alifichua kashfa mbali mbali serikalini ikiwa ni pamoja na ile ya shirika la huduma ya vijana kwa taifa NYS na Eurobond. “Sidhani kama kuna anayeweza kufuata nyayo za Raila kati ya Musyoka, Wetangula na Mudavadi. Kumbuka ni Raila aliyekuwa akisukuma kubuniwa kwa mabunge ya wananchi yaliyokuwa yakikosesha Jubilee usingizi,” asema Bw Geff Kamwanah, mdadisi wa masuala ya kisiasa.

Anasema masuala ambayo NASA imekuwa ikipigania kama haki katika uchaguzi ni mazito na yanahitaji kiongozi mwenye ujasiri kama Raila.

Bw  Musyoka, Bw Wetang’ula na Bw Mudavadi wanasema wako tayari kusukuma ajenda za NASA bila Bw Odinga lakini hii ni kama mzaha,” asema mwanahabari na mdadisi wa masuala ya siasa Macharia Gaitho kwenye makala yaliyochapishwa katika gazeti la Daily Nation.”

“Wamekasirika kwa sababu Bw Odinga alizungumza na Bw Kenyatta bila kuwahusisha,” alisema Bw Gaitho.

Bw Kamwanah anasema ishara kwamba Musyoka, Wetangula na Mudavadi hawana ujasiri wa kukabiliana na serikali ni kujitenga kwao na Raila alipokula kiapo kama rais wa wananchi.

“Huo ulikuwa mtihani waliofeli. Raila amejaribiwa mara nyingi kwa moto, ameteswa na kutupwa jela na kuibuka jasiri zaidi. Kwa kuzika tofauti zake na Rais Uhuru ni kama kuua upinzani,” aeleza.

Raila amesisitiza kuwa hajahama NASA akisema muafaka wake na Rais Kenyatta ni wa watu wawili na sio mirengo ya kisiasa. Hata hivyo, matamshi yake na washirika wake wa kisiasa, wakiwemo wabunge wa chama cha ODM, yanatoa ujumbe tofauti. Kulingana na mbunge wa Lugari Ayub Savula, Wiper, ANC na Ford Kenya viko tayari kuunda upinzani rasmi bila ODM.”

ODM ikioana na Jubilee tuko tayari kuunda upinzani rasmi,” alisema. Hata hivyo, wadadisi wanasema wanachotaka wabunge hao wapatao 40 bila ODM ni vyeo vya upande wa upinzani bungeni.

“Kenya imerejea ilipokuwa 1997 upinzani ulipodhoofishwa Raila alipojiunga na serikali ya Kanu. Jukumu la kukosoa serikali lilichukuliwa na vyombo vya habari na mashirika ya kijamii na yasiyo ya Serikali.

Jinsi hali ilivyo wakati huu, uhuru wa wanahabari na mashirika ya kijamii umedidimizwa. Kwa ufupi, hakutakuwa na upinzani Kenya iwapo Raila atamezwa na Jubilee,” asema Bw Kamwanah.

Hisia za wadadisi ni kuwa, muafaka wa Raila na Uhuru ulipangwa ili  kupangua upinzani ukose makali ya kukosoa Serikali.

You can share this post!

Jirongo asimulia Raila alivyomsaidia kupata kazi Tanzania

JAMVI: ‘Jenerali’ kutua nchini bila gwaride wala...

adminleo