• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 10:08 PM
Joho ataka Raila aunge Mpwani kuwania urais

Joho ataka Raila aunge Mpwani kuwania urais

STEPHEN ODUOR na MOHAMED AHMED

GAVANA wa Mombasa, Hassan Joho ameeleza matumaini kwamba Kiongozi wa ODM, Bw Raila Odinga, ataunga mkono mgombeaji urais kutoka Pwani katika Uchaguzi Mkuu ujao.

Huku akiwajibu mahasimu wake wa kisiasa wanaoegemea upande wa Naibu Rais William Ruto, gavana huyo aliye pia naibu kiongozi wa ODM alisema Pwani itakuwa na mgombeaji urais mwaka wa 2022 na anaamini Bw Odinga ataunga mkono mgombeaji atakayetajwa.

Kulingana naye, eneo hilo limekuwa likimuunga mkono Bw Odinga kwa muda mrefu kwa sababu waziri mkuu huyo wa zamani anajua eneo hilo linatarajia atarudisha mkono.

Kufikia sasa, Bw Odinga hajatangaza iwapo atawania urais katika uchaguzi ujao huku Bw Joho akiwa tayari ameeleza azimio lake kuwania wadhifa huo.

“Hatuwezi kuunga mkono watu wengine kila mwaka wa uchaguzi. Tunataka kukaa kwenye meza. Hatuwezi kuendelea kuwa menyu. Hatuwezi kuwa katika hali ambapo wakati wowote kuna mipango inayofanywa, hakuna hata mmoja wetu kutoka eneo letu aliyepo. Hatuwezi kuendelea kuwakilishwa. Huu ni wakati wa kiongozi kutoka eneo hili kuwa kwenye debe la urais na matokeo ya kinyang’anyiro hicho yaamuliwe mbele mbele hata iweje,” akasema.

Hata hivyo, alionya kwamba hilo halitawezekana iwapo viongozi wa eneo hilo wataendelea kujibizana kwa njia inayoashiria ubinafsi.

Alisema mfumo wa siasa za Pwani unapaswa kuwa tofauti, kwa hivyo viongozi hawapaswi kuwa wepesi kutoa wito kwa umoja wa mkoa huo bila mipango kabambe.

“Hatutafanikiwa ikiwa tutaonekana kutoelewa kile tunachohitaji kama eneo,” alisema hayo wakati wa ziara katika Kaunti ya Tana River.

Aliwakashifu viongozi wa Pwani wanaoegemea upande wa Naibu Rais akisema wana nia mbaya wanapodai kwamba wanataka kuwaunganisha Wapwani.

Kwa mujibu wa Bw Joho, umoja wa Pwani haupaswi kuwa kwa msingi wa kuunga mkono kiongozi mmoja, bali kwa madhumuni ya kuwafaidi watu wa Pwani na kutatua changamoto wanazokabiliana nazo.

“Hatupaswi kuambiwa kwamba tunahitaji kuungana kwa sababu ya kiongozi fulani. Ikiwa tunatafuta umoja, basi iwe kwa mkoa wetu na kwa ajili ya Wapwani. Tunapaswa kuungana kwa sababu ya changamoto tunazokabiliana nazo kama wakaaji wa eneo hili,” alisema Bw Joho.

Wito kuhusu uundaji wa chama kimoja cha Wapwani umeshika kasi tangu uchaguzi mdogo wa Msambweni ufanyike, ambapo ODM ilishindwa na upande wa Dkt Ruto licha ya kutarajiwa na wengi kunyakua kiti hicho.

Matokeo hayo yalifanya baadhi ya viongozi wa eneo hilo kumtaka Gavana wa Kwale, Bw Salim Mvurya, atwikwe jukumu la kutoa mwelekeo wa kisiasa kwa Wapwani. Jukumu hilo limekuwa mikononi mwa Bw Joho kwa muda mrefu.

Wabunge wasiopungua 11 wa Pwani na Seneta wa zamani wa Mombasa Hassan Omar ambao wanamuunga mkono Dkt Ruto ndio wako katika mstari wa mbele kushinikiza kuundwa kwa mavazi mapya ya kisiasa kabla ya mwaka wa 2022.

You can share this post!

Kenya kuandaa mashindano ya kimataifa ya tenisi kwa...

UDA chajiuza kama chama kisichobagua Mkenya yeyote