• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 2:19 PM
Joho atiwa presha atangaze mrithi wake

Joho atiwa presha atangaze mrithi wake

Na WINNIE ATIENO

GAVANA wa Mombasa, Bw Hassan Joho amepuuzilia mbali shinikizo la wanasiasa wanaomtaka atangaze ni nani ambaye angependa awe mrithi wa kiti chake, akiwaambia wanaomezea mate kiti hicho wajitetee wenyewe kwa wananchi kabla ya uchaguzi mkuu ujao.

Kiti hicho kimevutia wanasiasa watano kufikia sasa wakiwemo Mbunge wa Mvita, Abdulswamad Nassir (ODM), mwenzake wa Kisauni, Ali Mbogo (Wiper), Naibu Gavana wa Mombasa, Dkt William Kingi (ODM), mfanyabishara Suleiman Shahbal (ODM) na aliyekuwa seneta wa Mombasa, Bw Hassan Omar ambaye ni mwandani wa Naibu Rais William Ruto.

Akiongea jana wakati wa maadhimisho ya Siku ya Utalii Ulimwenguni katika Hoteli ya Pride Inn eneo la Shanzu, Bw Joho aliwapuuzilia mbali baadhi ya wanasiasa walioanza kujipigia debe wakionekana kutaka baraka zake.“Ndugu zangu ambao mnagombea, ninawatakia kila la heri. Mungu awaongoze,” akasema.

Baadhi ya waliojipigia debe mbele yake ni Dkt Kingi na Bw Nassir, lakini Bw Joho aliwataka waeneze sera zao na kuhakikisha wanadumisha amani katika kampeni.

Alizidi kuwashauri kuwa wahakikishe kampeni zao hazitasababisha mgawanyiko wa kikabila Mombasa kwani wakazi wa makabila tofauti wameishi hapo kwa amani kwa miaka mingi sasa.

Dkt Kingi alimsifu Bw Joho akisema amefanya kazi nzuri kwenye uongozi wake wa mihula miwili akisisitiza kuwa yeye ndiye anayefaa kuendeleza ajenda zake.

“Mimi ndiye ninayefaa kumrithi ili nimalize miradi mikuu ambayo tulianza. Bw Joho aliingia uongozini na kutatua changamoto ya usalama. Hivi sasa tunasherehekea amani kwa sababu ya juhudi zake sawia na kuleta uwiano,” alisema Dkt Kingi.

Kwa upande wake, Bw Nassir alipinga madai kuwa amejiuzulu kwenye kinyang’anyiro hicho na kumwachia Bw Shahbal baada ya kushawishiwa na Bw Odinga na Bw Joho. Hii ni baada ya tetesi kuibuka kuwa Bw Nassir alikubali kuwania useneta badala ya ugavana.

“Huo ni uongo na uzushi. Bado nawania ugavana,” akasema. Wakati huo huo, Bw Joho alitetea uongozi wake kwa kupigania maslahi ya wakazi hasa baada ya wakosoaji wake kumlaumu kuhusu suala la kudorora kwa uchumi wa jiji hilo.

Alimshtumu Dkt Ruto kwa kuwahadaa Wakenya na kumwita kwamba yeye ni ‘mjinga’ alipotoa taarifa kuhusu kuhamishwa kwa bandari ya Mombasa hadi Naivasha.“Sasa wao ndio wanaopiga kelele wakijifanya watakatifu wakiwaelezea vile nyinyi ni maskini.

Alipokuwa kwenye meza ya uongozi hakutamka anayoyasema hivi sasa. Amkeni ndugu zangu msilale, msikubali kuhadaiwa. Mbona hakuleta mabadiliko hapo awali alipokuwa na uwezo?” aliuliza.

Alisifu maridhiano kati ya Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa chama cha ODM Bw Raila Odingaakieleza namna kaunti ya Mombasa ilivyofaidi kwa mazuri ikiwemo ujenzi wa mabarabara.

You can share this post!

Miswada yataka walioshtakiwa wasiwanie viti

Viongozi Mlima Kenya wampa Raila matakwa