NA MOSES NYAMORI
KAMATI ya Mazungumzo ya Kitaifa yenye wanachama 10 iliyoundwa na Rais William Ruto na kiongozi wa Upinzani Raila Odinga, itatumia Sh106 milioni kufanikisha mazungumzo hayo ya maridhiano.
Bajeti iliyotayarishwa na sekretarieti na kupitishwa na Kamati ya Kitaifa ya Majadiliano inaonyesha kwamba sehemu kubwa ya mamilioni ya fedha imetengwa kwa ajili ya marupurupu ya wanachama na kuendeleza mikutano ya Naivasha na Mombasa.
Hati hiyo inaonyesha kuwa ushirikishi wa wadau unaoendelea ulioanza Jumatatu na unaopangwa kuendelea hadi Ijumaa, utatumia kiasi kikubwa cha fedha hizo kwa marupurupu, vifaa vya mikutano na viburudisho.
Harakati hii itatumia Sh5,996,000.
Kadhalika, ripoti hiyo pia inaonyesha kuwa Sh10 milioni nyingine zitatumika katika ‘kufasiri hati’ huku uchapishaji wa nakala 1000 ukigharimu Sh15,000,000.
Sh9.7 milioni zimetengwa kwa ajili ya dharura, ikiwa ni asilimia 10 ya gharama zote.Wenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Majadiliano – kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka na Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa Kimani Ichung’wah – wana haki ya kupata marupurupu ya Sh50,000 kwa kila kikao.
Hati ya bajeti inaonyesha kuwa Bw Musyoka na Bw Ichung’wah watahudhuria jumla ya vikao 20; vikao 15 katika ukumbi wa Bomas of Kenya, vitatu Naivasha wakati wa kuandika ripoti na viwili Mombasa wakati wa kupitishwa kwa hati ya mwisho itakayowasilishwa Bungeni.
Hii ina maana kuwa kila kiongozi atapata Sh2 milioni.
Hii itakuwa juu ya gharama nyinginezo kama vile tikiti za ndege na malazi zinazofikia maelfu ya pesa kwa kila mkutano uliopangwa Naivasha na Mombasa.
Wajumbe wengine wanane – Kiongozi wa Wengi katika Seneti Aaron Cheruiyot, Gavana wa Embu Cecily Mbarire, Mbunge wa EALA Hassan Omar, Mwakilishi wa Kike Catherine Wambilianga, Kiongozi wa Wachache Opiyo Wandayi, Kiongozi wa Chama cha DAP Eugene Wamalwa, Seneta wa Nyamira Okon’go Omogeni na Mbunge wa Malindi Amina Mnyazi watapata Sh40,000 katika kila kikao.
Wanane hao pia watahudhuria jumla ya vikao 20.
Wanachama pia watalipiwa gharama nyingine kama vile tikiti za ndege na malazi wakati wa mapumziko yaliyopangwa.
Wanachama wa kikosi cha wataalamu wanane wanaojumuisha wakili wa Mahakama Kuu Muthomi Thiankolu, Dkt Linda Musumba, wakili Nick Biketi, Dkt Duncan Ojwang, Katibu Mkuu wa Jubilee Jeremiah Kioni, Dkt Adams Oloo, aliyekuwa Mbunge wa EALA Zein Abubakar na Isabel Githinji pia watapokea Sh25, 000 kwa kila kikao kila mmoja.
Subscribe our newsletter to stay updated