WANGU KANURI Na RUTH AREGE
KIONGOZI wa chama cha Narc Kenya, Bi Martha Karua amesema kuwa, bado hajamtambua Dkt William Ruto kama rais.
Akizungumza kwenye mahojiano na shirika la habari la BBC, Bi Karua alisema, “Sheria imemkubali Ruto lakini mimi bado.”
Bi Karua ambaye alikuwa mgombea mwenza wa Raila Odinga katika muungano wa Azimio La Umoja-One Kenya alisisitiza kwamba, kuheshimu uamuzi wa Mahakama ya Upeo hakufai kuchukuliwa kama kutambua ushindi wa Rais Ruto.
“Tulisema kwamba tuliheshimu uamuzi wa Mahakama na yenyewe inajua kilichoendelea huko, hatukukubaliana nao,” alisema.
Mbunge huyo wa zamani wa Gichugu alisema siku moja ukweli utajulikana kuhusu kilichofanyika akishikilia kuwa uchaguzi wa urais ulikumbwa na dosari zinazopaswa kurekebishwa.
Akizungumza na mwanahabari Hassan Arouni wa kitengo cha Focus on Africa, Bi Karua ameendelea kusisitiza kuwa atawasilisha kesi mahakamani kutafuta haki.
Alisema kwa sababu Mahakama ya Upeo ya Kenya “ilishindwa kulinda demokrasia, watawasilisha kesi katika Mahakama ya Haki ya Afrika Mashariki ili kulinda na kutia nguvu taasisi na asasi za nchi”.
Alipoulizwa kuhusu uwezekano wa kufanya kazi kwa karibu na Rais Ruto aliashiria kuwa hilo halitawezekana.
“Sijakuwa serikalini kwa miaka 10, lakini sauti yangu imekuwa ikisikika. Na hivi sasa sauti yangu inaendelea kusikika,” alisema.
Subscribe our newsletter to stay updated