NA BENSON MATHEKA
MGOMBEAJI urais kwa tikiti ya wa Muungano wa Azimio la Umoja One Kenya kwenye uchaguzi mkuu uliopita, Raila Odinga, amerudi mitaani kujumuika na wananchi wa mapato ya chini maarufu kama mahasla, katika moja ya hatua zake za kutekeleza mikakati ya kutoa jasho serikali ya Kenya Kwanza.
Bw Odinga aliyeshindwa na Rais William Ruto kwenye uchaguzi huo wa Agosti 9, ametangaza kwamba, atakuwa msitari wa mbele kutetea demokrasia ambayo alikuwa miongoni mwa viongozi walioipigania na ambayo anahisi inatishiwa.
“Tuko na kazi ya kufanya. Kusalimu amri sio msamiati katika mageuzi yetu. Tuko na jukumu kama watu kutia nguvu ufanisi wetu na kusimama imara,” Bw Odinga alisema wakati wa hafla ya kuzindua kitabu cha Mkurugenzi Mkuu wa ODM Bw Oduor Ong’wen.
“Vijana wetu wengi hawajui kilichofanyika katika nchi yetu. Wanajiita mahasla kwa sababu hawajui. Tuko tulipo kwa sababu watu waliteseka na baadhi wakafariki kwa ajili ya demokrasia. Na kama haitalindwa, basi tunaweza kurudi tulikotoka,” alisema Raila.
Siku chache baada ya tamko hilo, Bw Odinga amekuwa akionekana katika mitaa ya jiji la Nairobi akijumuika na walala hoi katika kile alichotaja kama “ziara za kukutana na wafuasi wake kuwafariji kwa hali ngumu ya maisha inayowakabili.”
Mnamo Jumatano, Bw Odinga alizuru maeneo bunge ya Ruaraka na Mathare jijini Nairobi ambapo alijumuika na vijana na akina mama mboga.
Katika ziara hiyo, alikashifu serikali ya Kenya Kwanza kwa kushindwa kupunguza gharama ya maisha alivyoahidi kiongozi wake William Ruto wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu.
“Gharama ya maisha iko juu sana kiasi cha kuwalemea Wakenya wa kawaida. Wakati umefika sasa kwa hatua zichukuliwe kupunguzia raia mzigo huu,” alisema Bw Odinga.
Mnamo Jumanne, Bw Odinga alitangamana na wananchi wa kawaida katikati mwa jiji la Nairobi na hata akawashangaza wanabodaboda kwa kuwapa Sh20,000 wanunue petroli.
Siku hiyo, waziri mkuu huyo wa zamani alitembea kwa miguu katika barabara kadhaa za jiji hadi bustani ya Jevanjee kukutana na wanachama wa Bunge la Wananchi ambapo aliwataka mahasla kusimama imara kulinda haki zao za kikatiba.
“Nawahimiza msimame imara kulinda haki zetu za kikatiba. Uhuru wa kukutana na kujieleza ni nguzo muhimu ya demokrasia yetu,” Bw Odinga aliambia Bunge la Wananchi, kikundi cha wananchi wa kawaida kinachojadili masuala ibuka yanayoathiri mwananchi wa kawaida.
Bunge la Wananchi lilikuwa katika mstari wa mbele wakati wa kupigania siasa za vyama vingi na katiba mpya iliyopitishwa 2010.
Duru ndani ya Azimio zinasema, Bw Odinga anapanga kuhamasisha Wakenya wa mapato ya chini waweze kushinikiza serikali kuwatimizia ahadi ilizowapa wakati wa kampeni huku akianika maovu ya utawala wa Rais William Ruto bila kuzua fujo.
“Tarajia kumuona katika maeneo tofauti ya nchi akikutana na raia wa kawaida anaoamini wanahitaji kufahamishwa ukweli kuhusu yanayoendelea katika serikali,” alisema mbunge mmoja wa Azimio aliyeomba tusitaje jina kwa kuwa haruhisiwi kuzungumzia mikakati ya muungano huo.
Bw Odinga ameapa kuongoza wafuasi wake kupigania mageuzi ya mfumo wa uchaguzi, mageuzi ya kiuchumi na idara ya mahakama kuhakikisha kila Mkenya anapata haki.
Subscribe our newsletter to stay updated