• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 9:50 AM
Ramadhan kupiga breki siasa moto za kumrithi Joho

Ramadhan kupiga breki siasa moto za kumrithi Joho

Na MOHAMED AHMED

MFUMO wa mwezi mtukufu wa Ramadhan unatarajiwa kutuliza kasi ya siasa za urithi wa kiti cha ugavana cha Mombasa ambazo zimepamba moto.

Kindumbwendumbwe hicho kinatarajiwa kuibuka upya baada ya Ramadhan ambayo itadumu mwezi mmoja.

Siasa hizo za urithi wa Gavana Hassan Joho zimekuwa zikiendelea chini kwa chini licha ya shughuli za kisiasa kuonekana kupungua katika kaunti hiyo.

Kufikia sasa, Mbunge wa Mvita Abdulswamad Nassir, Mbunge wa Kisauni Ali Mbogo na mfanyabiashara Suleiman Shahbal ndio viongozi ambao wamejitosa ulingoni wazi wazi wakitaka kumrithi Gavana Hassan Joho.

Hata hivyo, ushindani mkali unatarajiwa kati ya Bw Nassir na Bw Shahbal ambao ndio mahasimu wakuu.

Huku Bw Nassir akionekana kuidhinishwa na Bw Joho katika azma yake, Bw Shahbal ambaye pia sasa ana uhusiano wa karibu na Bw Joho amekuwa akiendeleza kampeni za mapema kupitia vikao vinavyotambulika kama “Gumzo Maskani”.

Kati ya Februari na mwezi jana, kiongozi huyo aliandaa mikutano kadhaa katika maeneo bunge ya Mombasa ikiwemo Likoni, Changamwe, Mvita Kisauni na Jomvu kunadi sera zake.

Bw Nassir naye kwa upande wake amekuwa akitumia nafasi yake kama kiongozi kukutana na wakazi hususan wa eneo bunge lake la Mvita na kuvumisha azma yake ya kutaka kuwania ugavana.

Hata hivyo, Bw Nassir hajakuwa akitembelea maeneo bunge mengine kufanya kampeni zake sawa na Bw Mbogo ambaye pia ameshikilia kampeni zake mashinani katika eneo bunge lake la Kisauni.

Uchunguzi wa Taifa Leo umeonyesha, katika miezi hiyo miwili iliopita, Bw Nassir amezuru makanisa katika eneo la Changamwe mara tatu huku Bw Shahbal akiandaa mikutano takribani 20 katika muda huo huo.

Kampeni hizo za mapema pia zimeibua tumbojoto katika chama cha ODM baada ya Bw Shahbal kutangaza kuwa anarudi katika chama hicho.

“Walinifungia mlango wakati ule lakini sasa si handisheki imekuja. Si tumerudi nyumbani?” Bw Shahbal alisema katika mmoja wa mikutano yake.

Tangazo hilo la Bw Shahbal lilipelekea Bw Nassir naye kumpiga vijembe mpinzani wake huyo na katika mkutano wa eneo la Jomvu akaonya wakazi dhidi ya kuchagua watu ambao wanajitokeza wakati huu.

“Nawauliza, wao walikuwa wapi wakati sisi tulikuwa tunapambana? Mimi nawaambia muwe makini na watu hao,” akasema Bw Nassir.

Licha ya wawili hao kujitokeza katika kumenyania kiti hicho, bado haijakuwa wazi iwapo Bw Joho atamuunga mkono yeyote kati yao.

Iwapo Bw Joho atajitokeza wazi kumuunga mkono kiongozi wa kumrithi, basi naibu wake Dkt William Kingi atakuwa miongoni mwa wale wanaotarajia kuungwa mkono.

Dkt Kingi pia amewahi kutangaza kuwa atawania kiti cha ugavana, hata hivyo hakuna mikutano yoyote ya wazi ya kampeni ambayo ameanza kuandaa.

Aliyekuwa seneta wa Mombasa Hassan Omar pia anatarajiwa kushiriki kwenye kinyanganyiro hicho. Hata hivyo, bado pia yeye hajaanza kujitosa kwenye kampeni za mapema.

You can share this post!

Msomi akiri kukiuka maadili kwenye mahojiano ya Jaji Mkuu

Viongozi wa ODM wataka Obado atimuliwe chamani