• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 6:47 PM
Riggy G akutana na wabunge wa Jubilee kutoka Mlima Kenya kuimarisha ndoto yake ya kuwa ‘mfalme’ wa siasa za eneo hilo

Riggy G akutana na wabunge wa Jubilee kutoka Mlima Kenya kuimarisha ndoto yake ya kuwa ‘mfalme’ wa siasa za eneo hilo

Na CHARLES WASONGA

NAIBU Rais Rigathi Gachagua Ijumaa jioni alikutana na wabunge waliochaguliwa kwa tiketi ya chama cha Jubilee katika afisi yake iliyoko katika Jumba la Harambee House Annex.

Japo mkutano huo ulisemekana kuitishwa kwa lengo la kujadili masuala ya maendeleo, duru zilisema mada za kisiasa pia zilijadiliwa.

Aidha, mkutano huo unaonekana kama sehemu ya juhudi za Gachagua kujikuza kama kinara wa siasa za Mlima Kenya, ikizingatiwa kuwa ni wabunge Jubilee kutoka eneo hilo ndio waliuhudhuria.

“Leo, niliwakaribisha Wabunge kutoka Jubilee, chama chetu cha zamani, katika Harambee House Annex. Tulijadili masuala yanayohusiana na maendeleo katika maeneo wanayowakilisha,” akasema Bw Gachagua kupitia akaunti yake ya Twitter.

“Uchaguzi umeisha, na sharti tufanye kazi pamoja bila kujali miegemeo yetu ya kisiasa. Kwa hakika, Mheshimiwa Rais William Ruto na mimi tumekubaliana kwamba 2023 ni mwaka wa kazi, na sharti tuweke masilahi ya watu mbele kwanza ili kujenga upya uchumi wetu,” akaongeza.

Miongoni mwa waliohudhuria mkutano huo ni Mbunge Maalum Sabina Chege, na Mbunge wa Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) Kanini Kega.

Pia wabunge wanaowakilisha maeneo bunge walikuwepo, wao ni : David Kiaraho (Ol Kalou) Irene Njoki (Bahati), Zachary Kwenya (Kinangop), Dkt Shadrack Mwiti (Imenti Kusini ), Mark Mwenje (Embakasi Magharibi), Amos Mwago (Starehe), Dan Karitho (Igembe ya Kati), Stanley Muthama (Lamu Magharibi)  na Seneta wa Lamu Joseph Githuku.

Lakini japo, mkutano huo ulisemekana kati ya Bw Gachagua na wabunge wa chama cha Jubilee, ambacho ni chama tanzu katika muungano wa Azimio wabunge wa chama hicho kutoka maeneo yaliyoko nje ya Mlima Kenya hawakuhudhuria.

Wao ni pamoja na Mbunge wa Sirisia John Waluke na mwenzake wa Eldas Aden Keynan.

  • Tags

You can share this post!

Macho kwa Ruth Chepng’etich watimkaji 400 wakishiriki...

West Ham United wajinasia huduma za Danny Ings kutoka Aston...

T L