• Nairobi
  • Last Updated May 7th, 2024 5:55 PM
Ruto hatimaye afafanua mfumo wa ‘Bottom-up’

Ruto hatimaye afafanua mfumo wa ‘Bottom-up’

Na WANDERI KAMAU

NAIBU Rais William Ruto hatimaye amejitokeza kutetea mpango wake wa kiuchumi wa kuwainua watu maskini maarufu kama Bottom Up Model baada ya wandani wake kadhaa kuonekana kushindwa kuufafanua inavyofaa.

Baadhi ya washirika wa Dkt Ruto wamejipata matatani, wakishindwa kueleza kwa kina maana halisi ya mfumo huo.

Miongoni mwa wale waliojipata katika hali hiyo ni mbunge Alice Wahome (Kandara) na Kimani Ichung’wa (Kikuyu).

Kwenye mahojiano na kituo kimoja cha televisheni mapema wiki hii, Bi Wahome alionekana kushindwa kabisa kufafanua jinsi mpango huo utakavyowasaidia Wakenya ikiwa Dkt Ruto atachaguliwa kuwa rais kwenye uchaguzi mkuu wa 2022.

Bw Ichung’wa pia alijipata katika hali iyo hiyo majuzi, alipoelezwa kutofautisha mfumo huo na ule wa ugatuzi, kwani utaratibu wake ni kuelekeza fedha mashinani.

Lakini jana, Dkt Ruto alisema kuwa mpango huo unalenga kuwasaidia wananchi wa kiwango cha chini, kuwawezesha kuendesha biashara zao bila kuchukua mikopo kutoka kwa wakopeshaji wa kibinafsi na mashirika mengine ya kifedha yanayowatoza riba ya kiwango cha juu.

“Lengo letu ni kuwainua wananchi wa kiwango cha chini kwa namna ambayo wataweza kujisimamia kifedha kwa kupata mikopo ya riba ya kiwango cha chini. Tutaafikia hili kwa kubuni hazina maalum kushughulikia mahitaji yao ya kifedha,” akasema Dkt Ruto.

Baadhi ya viongozi wamekuwa wakikosoa mfumo huo kama unaokosa kueleza kwa kina jinsi utakavyowainua Wakenya.

Hapo awali Naibu Rais alikuwa ameahidi kutenga takribani Sh200 bilioni kutoka kwa mgao wa maendeleo kwenye bajeti ili kuinua biashara za kiwango cha chini.

You can share this post!

Hatimaye Moi atangaza kuwania urais 2022

Bei ya chai sasa yapanda kanuni mpya zikianza kuzaa matunda