NA WANDERI KAMAU
WANASIASA waasi katika Chama cha Jubilee wamesema kuwa Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta anafaa kuwashukuru, kwa kujitolea kumfanyia kampeni kwenye Uchaguzi Mkuu wa 2022 badala ya kuwalaumu.
Mnamo Ijumaa, wanasiasa hao walisema ni kosa kubwa kwa Bw Kenyatta kuwalaumu kwa “usaliti”, ilhali baadhi yao walipoteza viti vyao vya kisiasa kwa kuunga mkono mrengo wa Azimio la Umoja.
Kwenye uchaguzi huo, Bw Kenyatta alimpigia debe na kumuunga mkono kiongozi wa mrengo huo, Bw Raila Odinga, kuwania urais.
Kwenye mahojiano na kituo kimoja cha televisheni, Ijumaa asubuhi, Mbunge Maalum Sabina Chege, alisema Bw Kenyatta ndiye anafaa kuwashukuru, kwani baadhi ya viongozi walipoteza nafasi zao kutokana miegemeo yao ya kisiasa wala si kutokana na utendakazi mbaya.
“Ni kosa Bw Kenyatta kutulaumu licha ya kujiweka hatarini kisiasa kumpigia debe mtu aliyemuunga mkono kuwania urais. Binafsi, najutia baadhi ya maamuzi niliyofanya, kwani ningekuwa mtu mkubwa sana katika siasa kwa sasa. Baadhi ya wabunge wangehifadhi viti vyao, japo walikosa kuchaguliwa kama “adhabu” ya kuunga mkono Azimio,” akasema Bi Chege.
Akaongeza: “Ni jambo lipi linalozidi kuhatarisha mustakabali wako kisiasa kwa manufaa ya mtu mwingine? Tunafaa kupewa shukrani.”
Kauli ya Bi Chege inaonekana kama jibu kwa Bw Kenyatta, ambaye Ijumaa alishikilia kwamba “hatawaruhusu waasi kumnyang’anya udhibiti wa Jubilee”.
Bw Kenyatta alidai kuwa wanasiasa hao wamefadhiliwa na serikali ya Kenya Kwanza “kumnyang’anya” chama hicho kwa nguvu.
“Hapo awali, nilikuwa tayari kukabidhi Jubilee kwa uongozi mpya. Hata hivyo, nimebadilisha msimamo wangu kutokana na yale yanayoendelea. Sitakikabidhi chama kwa kundi la wanasiasa waliofadhiliwa na serikali wanaotaka kukichukua kwa nguvu,” akasema.
Subscribe our newsletter to stay updated