NA SAMMY WAWERU
SHUGHULI ya kujumlisha kura eneobunge la Kieni, Kaunti ya Nyeri inaendelea siku moja baada ya taifa kushiriki uchaguzi mkuu, Agosti 9.
Zoezi hilo lilianza mapema Jumatano, na kufikia sasa foleni ya masanduku ya kura ambazo hazijajumlishwa ingali ndefu.
Linafanyika katika kituo kikuu cha kujumlisha kura, kilichoko Shule ya Upili ya Mweiga.
Eneobunge la Kieni lina idadi jumla ya vituo 232 vya kupigia kura.
Afisa wa IEBC anayesimamia shughuli hiyo (R.O), Bw David Mbui ameambia Taifa Leo huenda ikaendelea hadi kesho, Alhamisi.
Masanduku yote hata hivyo yamewasili.
Hayo yakiendelea, mbunge wa sasa Kieni, Kanini Kega amekubali kushindwa kuhifadhi kiti chake hata kabla ya matokeo rasmi kutangazwa na IEBC.
Bw Kega alitoa tangazo hilo kupitia akaunti zake za mitandao ya kijamii, akisema “nimefungua chapta nyingine, mlango mmoja unapofungika mwingine hufunguka…”
Mbunge huyo anayeondoka aliwania kutetea wadhifa wake kupitia tiketi ya Jubilee.
Alimenyana na mgombea wa UDA, Wainaina Njoroge.
Kura zikiendelea kujumlishwa, zinaashiria Bw Njoroge huenda akatwaa kiti cha ubunge Kieni.
Hali ya usalama imeimarishwa Shule ya Upili ya Mweiga, vikosi vya pamoja vya askari vikishika doria kila pembe ya mazingira.