• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 3:55 PM
Uozo wa kimaadili miongoni wa wabunge waanikwa

Uozo wa kimaadili miongoni wa wabunge waanikwa

Na CHARLES WASONGA

HUKU Spika wa Bunge Justin Muturi akiahidi kuwa madai ya ufisadi yaliyoelekezewa wabunge fulani na kampuni moja ya kutengeneza mvinyo yatachunguzwa imebainika kuwa wabunge hutumia kamati zao kama majukwaa ya kujitajirisha kinyume cha sheria.

Bw Muturi amethibitisha kupokea barua kutoka kwa mwenyekiti wa kampuni ya London Distiller Kenya Ltd (LDK) Mohan Galot, akilalamika kuwa wanachama wa Kamati ya Bunge kuhusu Utekelezaji walihongwa na kampuni ya nyumba ya Erdermann Property Ltd ili wapendekeze kufungwa kwake.

Kampuni hiyo inayomiliki mtaa wa makazi ya Great Wall Garden iliyoko Athi River ilidai kuwa LDK imekuwa ikiachilia maji taka katika mto Athi na hivyo kuhatarisha maisha ya wakazi. Madai hayo yalichunguzwa na Kamati ya Bunge kuhusu Mazingira na Mali Asili ambayo ilipendekeza kampuni ya LDK ifungwe ikiwa haitasita kuachilia maji taka katika mto Athi.

Katika barua yake kwa Muturi Bw Galot anasema hivi: “Wabunge wanachama wa kamati hiyo walipokea nyumba bila malipo au kwa bei nafuu kupitia jamaa zao au kampuni ambazo wao ni wakurugenzi ili wapendekeze kufungwa kwa LDK. Tunaomba afisi yake iwachukulie hatua wanachama wa kamati hii.”

“Malalamishi yaliwasilishwa na karani wa bunge alimwandikia mlalamishi akithibitisha kupokea barua yake. Suala hilo linachunguzwa,” Bw Muturi akasema.

Lakini mwenyekiti wa Kamati hiyo Moitalel Ole Kenta alipuuzilia mbali madai hayo akisema hayana msingi wala ukweli wowote.

“Tunataka yule aliyetoa madai hayo ya kiajabu kuyafafanua na kutoa ushahidi mbele ya asasi huru ya uchunguzi.” Akasema Bw Ole Kenta ambaye ni Mbunge wa Narok Kaskazini.

Bw Ole Lenta ameutaka usimamizi wa kampuni hiyo ya kutengeneza mvinyo kufika mbele ya Spika Muturi na ushahidi unaonyesha kuwa wanachama wa kamati yake walipokea hongo.

“LDK lazima ifike mbele ya kamati na kutaja majina ya wabunge inaodai kuwa walipewa nyumba. Hatujawahi kuhongwa na tutaendelea kufanya kazi yetu. Ripoti ya Kamati ya Mazingira lazima itekelezwe,” akasema mbunge wa Narok Kaskazini.

Alimshutumu Bw Galot kwa kujaribu kuwanyamazisha wanakamati.

“Kwake yeye maisha ya Wakenya wanaoathiriwa na uharibifu wa mazingira si muhimu. Kampuni hii ilifaa kufungwa miezi sita iliyopita kama tungetekeleza mapendekezo ya ripoti ya Kamati ya Mazingira. Tulisikiza vilio vya wafanyikazi na tukaipa LDK muda wa kutekeleza mapendekezo ya wabunge,” akasema Bw Ole Kenta.

Naibu mwenyekiti wa kamati hiyo, Bw Geoffrey Osotsi alisema wanachama wamekuwa wavumilivu na watatekeleza usawa kwa pande zote husika katika mzozo huo.

Mapendekezo ya Kamati ya mazingita yaliidhinishwa na Bunge mwaka 2018 kutokana na kesi iliyowasilishwa na Erdemann Ltd na wanunuzi 3,000 wa nyumba, waliolitaka Bunge lichunguze athari za shughuli za LDK kwa mazingira.

Madai ya ufisadi dhidi ya wanachama wa kamati ya bunge kuhusu utekelezaji ni mojawapo tu ya msusuru wa madai kama hayo ambayo yameshusha hadhi ya bunge.

Wabunge wamekuwa wakikashifiwa kwa kupokea mamilioni ya fedha ili kuwakinga maafisa wa umma wanaofika mbele ya kamati zao kuchunguzwa kuhusiana na tuhuma mbalimbali za ufisadi na uhalifu wa kifedha.

Wabunge wanachama wa kamati ambazo huchunguza ripoti za Mkaguzi wa Hesabu zinazofichua visa mbalimbali vya matumizi mabaya ya fedha za umma katika asasi za serikali na serikali za kaunti wameshutumiwa kupokea hongo ili kuwalinda maafisa husika au kuandika ripoti inayowaondolea lawama.

Vile vile, kumekuwa na madai ya wabunge kuhongwa ili kutupilia mbali ripoti ya kamati za bunge zinazopendekeza maafisa fulani wakuu serikali kuchukuliwe hatua za kisheria.

Kwa mfano, mnamo 2018, Kamati ya Bunge kuhusu Hadhi na Mamlaka ya Bunge chini ya uenyekiti wa Spika Muturi ilipendekeza kuita Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) ichunguze madai kuwa wabunge walihongwa kwa hadi Sh20,000 ili watupilie mbali ripoti kuhusu sakata ya uagizaji sukari yenye sumu.

Kiongozi wa wachache bunge John Mbadi aliungama kuwa madai hayo yana mashiko akisitikisha kuwa yanashusha hadhi ya bunge kama asasi ya kulinda masilahi ya raia.

“Uvumi kwamba wabunge wamekuwa wakihongwa una mashiko. Kwa mfano, kuhusu sakata ya sukari, ilidaiwa kuwa shahidi mmoja aliwahongwa wanachama wa kamati husika kwa Sh300,000 kila mmoja. Tunaambiwa kuwa afisa mwingine aliwapa baadhi ya wabunge Sh500,000 kila mmoja ili wamtetee,” akasema Mbadi ambaye ni Mbunge wa Suba Kusini.

Wakati wa sakata hiyo Mbunge wa Kimilili Didmus Barasa alidai kuwa Mbunge Mwakilishi wa Wajir Fatuma Gedi alijaribu kumhonga kwa Sh10,000 ndani ya ukumbi wa bunge ili kumshawishi aangushe ripoti hiyo ya sakata ya uagiza sukari.

Ripoti hiyo ilipendekeza kwamba aliyekuwa Waziri wa Biashara Adan Mohamed na aliyekuwa Waziri wa Fedha Henry Rotich wachukuliwe hatua za kinidhamu kwa kuruhusu kuingizwa nchini kwa sukari yenye sumu na bila kulipiwa ushuru inayohitajika.

Mbunge Mwakilishi wa Kiambu Gathoni Wa Muchomba alitoa madai ya kiajabu kwamba baada ya wabunge wa kike walikuwa wakipokezwa hongo zao msalani.

You can share this post!

UCL: Bayern na PSG kukabana tena

Equator Rally kushuhudia kivumbi kikali magari saba ya...