Alex Njeru na Reginah Kinogu
Mkutano ambao viongozi waliochaguliwa eneo la Mlima Kenya walipanga kuzindua chama kipya cha kisiasa umeahirishwa kwa wiki moja.
Mkutano huo uliokuwa umepangwa kufanyika leo katika uwanja wa michezo wa Karubia mjini Chuka uliitishwa na magavana Muthomi Njuki (Tharakanithi), Kiraitu Murungi (Meru) na Martin Wambora (Embu).
Spika wa bunge la kitaifa Justin Muturi na aliyekuwa seneta wa Embu Lenny Kivuti, wabunge na madiwani kadhaa pia walitarajiwa kuhudhuria mkutano huo.
Uamuzi wa kuahirisha mkutano huo uliafikiwa huku mazungumzo yakiendelezwa na viongozi na wataalamu kutoka eneo la kati ya Kenya kuwa na mwelekeo wa eneo hilo katika siasa za kitaifa na maendeleo.
Jana, Gavana Njuki alisema kwamba maslahi ya eneo wakazi wa Mlima Kenya Mashariki yanaweza kutimizwa kupitia umoja wa viongozi na sio kupitia watu ambao uaminifu wao uko kwingine.