• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 6:50 AM
Wakili Karim Khan kujiondoa kwenye kesi ya Ruto ICC

Wakili Karim Khan kujiondoa kwenye kesi ya Ruto ICC

Na VALENTINE OBARA

KIONGOZI wa Mashtaka katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC), Bi Fatou Bansouda, ametangaza kuwa wakili Karim Khan atakayechukua nafasi yake Juni atahitajika kutoshiriki katika kesi ambazo aliwahi kuwakilisha washtakiwa akiwa wakili.

Bw Khan alipata umaarufu humu nchini alipoongoza kikundi cha mawakili ambao walimwakilisha Naibu Rais, Dkt William Ruto aliyeandamwa na mashtaka kuhusu ghasia za baada ya uchaguzi wa 2007.

Ijapokuwa kesi ya Dkt Ruto ilisitishwa sawa na ile ya Rais Uhuru Kenyatta na mwanahabari Joshua Sang, majaji waliruhusu upande wa mashtaka kuzifufua endapo ushahidi mpya utapatikana baadaye.

Bw Khan alipigiwa kura kwa wingi mnamo Februari 12 na mataifa yaliyo wanachama wa ICC, ili kumrithi Bi Bensouda hatamu yake itakapoisha Juni 16.Alimshinda Bw Fergal Geynor aliyekuwa wakili wa waathiriwa wa ghasia za baada ya uchaguzi wa 2007. Serikali ilikuwa imepinga uteuzi wa Bw Geynor.

“Ninataka kuondoa hofu yoyote iliyopo kuhusu uwezekano wa Bw Khan kuwa na mapendeleo atakapohudumu kama kiongozi mpya wa mashtaka ICC. Katika mawasiliano yetu, alinihakikishia kuwa hatasimamia kesi yoyote ambayo aliwahi kuwakilisha washtakiwa au washukiwa,” Bi Bensouda akasema katika taarifa Ijumaa.

Kwa sasa mahakama hiyo inaendeleza kesi dhidi ya wakili Paul Gicheru anayedaiwa kushawishi mashahidi kujiondoa katika kesi iliyomwandama Dkt Ruto.

Bi Bensouda alieleza kuwa waandishi wa sheria zinazotumiwa ICC walitabiri uwezekano wa wakili wa washtakiwa kuajiriwa baadaye kuhudumu katika afisi ya kiongozi wa mashtaka ndiposa wakabuni sheria inayopiga marufuku kiongozi wa mashtaka na naibu wake kushiriki katika kesi yoyote ambayo itaibua hofu ya mapendeleo kutoka kwao.

“Bw Khan atatimiza hitaji hilo la kisheria kila wakati atakapohitajika kufanya hivyo,” akasema.Kesi ya Dkt Ruto ilisitishwa Aprili 2016 baada ya upande wa mashtaka kuambia mahakama kuwa hapakuwa na ushahidi wa kutosha.

Bi Bensouda alidai hili lilisababishwa na jinsi mashahidi wengi walivyoshawishiwa kujiondoa huku wengine wakitoweka kwa njia zisizoeleweka.

Upande wa mashtaka pia ulidai kuwa serikali ya Kenya ilikataa kusaidia katika ukusanyaji wa ushahidi zaidi uliohitajika.Hata hivyo, madai hayo yalipuuziliwa mbali na Dkt Ruto pamoja na mawakili wa serikali ambao walisisitiza kuwa upande wa mashtaka haukuwahi kuwa na ushahidi tangu kesi hizo zilipoanza chini ya aliyekuwa kiongozi wa mashtaka Louis Moreno Ocampo.

Kwingineko, kesi ya ulanguzi wa dawa za kulevya dhidi ya raia wa Tanzania aliyekamatwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Moi itatajwa leo katika Mahakama ya Mombasa.

Maimuna Jumanne Amir aliyekamatwa Machi 14 na kukaa korokoroni kwa siku nne, alifunguliwa mashtaka ya kukamatwa akiwa anasafirisha gramu 5,389 za heroini.

Mshukiwa alikanusha shtaka hilo alipofikishwa mbele ya Hakimu Mkuu Mkazi, Bw Vincent Adet.Polisi wanadai kuwa mtuhumiwa huyo alisafiri kutoka Afrika Kusini, kupitia Addis Ababa, Ethiopia kabla ya kutua nchini.

Alikamatwa siku chache baada ya watu wanne kukamatwa eneo la Mji wa Kale, Mombasa wakisafirisha kilo mbili za dawa ya heroini yenye thamani ya Sh6 milioni.

Maelezo zaidi na Brian Ocharo

You can share this post!

JAMVI: Raila anawazia nini iwapo atasalitiwa na Rais...

Fida-K yalalamikia ongezeko la mauaji ya wanawake Kenya