• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 11:34 AM
Mshukiwa wa nne wa wizi wa mabavu afikishwa kizimbani

Mshukiwa wa nne wa wizi wa mabavu afikishwa kizimbani

Na RICHARD MUNGUTI

SIKU arobaini zilitimia pale mshukiwa  wa nne aliposhtakiwa Jumanne  kwa kumshambulia na kumnyang’anya kimabavu mfanyabiashara Sh100,000 katika hoteli moja jijini Nairobi Aprili 30, 2018.

Bw Brian Shem Owino alifikishwa mbele ya hakimu mkuu katika mahakama ya Milimani Bw Francis Andayi. Alikanusha alimnyang’anya kimabavu Timothy Muriuki Sh100,000 katika hoteli ya Boulevard.

Shtaka lilisema wakati wa wizi huo mlalamishi alijeruhiwa.

Kiongozi wa mashtaka Bw Solomon Naulikha alimweleza hakimu kuwa kesi dhidi ya Bw Owino iunganishwa na nyingine dhidi ya Mbunge anayewakilisha Kenya katika bunge Afrika Mashariki (EALA) Simon Mbugua aliye na Mabw Antony Otieno  Ombok almaarufu Jamal na Benjamim Odhiambo Onyango almaarufu Odhis walifikishwa kortini baada ya patashika kadhaa kati ya polisi na washikadau wa haki waliotaka haki ifanywe na waliomshambulia Bw Timothy Muriuki wachukuliwe hatua kali.

Polisi waliwatia nguvuni watatu hao Mei 8 na kuwafungulia mashtaka.

Brian Shem Owino akiwa katika Mahakama ya Milimani. Picha/ Richard Munguti

Kisa hiki  cha kushambuliwa kwa Bw Muriuki kilipeperushwa katika vyombo vya habari na mitandao ya kijamii.

Washtakiwa waliomba waachiliwe kwa dhamana kupitia kwa mawakili Cliff Ombeta, Harun Ndubi,  Nelson Havi na Michael Osundwa.

Ijapokuwa ombi hilo lao halikupingwa na kiongozi wa mashtaka Solomon Naulikha , hakimu mwandamizi Martha Mutuku aliombwa awaachulie kwa masharti makali ikitiliwa maanani Bw Mbugua yuko na ushawishi mkubwa na atavuruga mashahidi.

Lakini Bi Mutuku aliwaachilia kwa dhamana ya Sh200,000 pesa tasilimu akisema “hakuna ushahidi uliowasilishwa kuonyesha kwamba washtakiwa wako na uhusiano na mashahidi.”

Korti ilisema mkurugenzi wa mashtaka ya umma DPP Noordin Haji anatakiwa kuwasilisha ushahidi kuhusu madai yanayotolewa kortini badala ya kuacha korti “ itegemee uvumi.”

Korti iliorodhesha kesi hiyo kusikizwa Julai 17.

Hakimu aliamuru kila mmoja wa washukiwa hao apewe nakala za mashahidi aandae utetezi wake.

You can share this post!

Maafisa 4 ndani miaka 3 kwa wizi na kutumia afisi...

Polisi wageukia Safaricom kupata taarifa kumshtaki...

adminleo