Na SAMMY WAWERU
SERIKALI inaendelea kutoa msaada wa chakula na mahitaji mengine muhimu ya kimsingi kwa familia zilizoathirika kufuatia kero ya uvamizi wa nzige.
Zaidi ya kaunti 32 zilikumbwa na nzige 2019 na 2020, maeneo kame yakiathirika pakubwa. Wadudu hao walishambulia mimea, mazao shambani na malisho ya mifugo, jamii zinazoishi maeneo yaliyoathirika zikikadiria hasara.
“Tunaendelea kutoa msaada wa chakula na mahitaji mengine muhimu ya kimsingi kwa walioathirika,” Katibu katika Wizara ya Kilimo, Mifugo na Samaki Prof. Boga Hamadi akaambia Taifa Leo Dijitali kupitia mahojiano ya kipekee jijini Nairobi.
Prof. Boga hata hivyo hakufichua idadi ya familia zilizoathirika kufuatia kero ya nzige. Mengi ya maeneo yaliyovamiwa na nzige yakiwa yale kame, yanaendelea kuhangaishwa na kiangazi, mifugo wakiripotiwa kufariki.
Zaidi ya kaunti 32 zilivamiwa na nzige. Serikali imethibitisha kufanikiwa kukabili kikamilifu wadudu hao waharibifu.