Na GEOFFREY ANENE
SHIRIKISHO la Mpira wa Magongo barani Afrika (AfHF) limetangaza orodha ya mataifa yatakayoshiriki Kombe la Afrika (makala ya 11 ya wanaume na makala ya nane ya kinadada) jijini Accra, Ghana mnamo Januari 17-23, 2022.
Kenya ya kocha Fidhelis Kimanzi, Misri, Ghana, Namibia, Nigeria, Afrika Kusini na Uganda zitawania ubingwa wa kitengo cha wanaume. Kinadada wa Kenya, ambao wanatiwa makali na Jacqueline Mwangi, watapigania taji dhidi ya Ghana, Namibia, Nigeria, Afrika Kusini, Uganda, Zambia na Zimbabwe.
Afrika Kusini imezoa mataji saba mfululizo ya wanaume ya Afrika tangu mwaka 1993 ikipiga Misri katika fainali ya makala matano yaliyopita. Kenya ilifika fainali ya dimba la wanaume mwaka 1974, 1983, 1989 na 1996. Katika makala yaliyopita mwaka 2017, Kenya ilikamata nafasi ya nne nyuma ya Afrika Kusini, Misri na Ghana mtawalia.
Kenya haijawahi kunyakua taji la kinadada. Ilipoteza 5-0 dhidi ya Afrika Kusini mara moja ilifika fainali mwaka 1998 jijini Harare, Zimbabwe. Kinadada wa Kenya walimaliza dimba hili katika nafasi ya nne nyuma ya Afrika Kusini, Ghana na Nigeria katika makala yaliyopita mwaka 2017, mtawalia.
Afrika Kusini imetwaa mataji sita mfululizo. Timu za Kenya, ambazo zimekuwa zikifanyia matayarisho yao ugani City Park jijini Nairobi, ziko jijini Mombasa kwa mashindano ya Daykio Japan Motors yaliyofahamika hapo awali kama SANA Cup.
|