KIBUKE, MAYANJA
NA DENNIS SINYO
MGANGA aliyekita kambi hapa alifunganya virago na kuondoka baada ya kukosa wateja kwa mwezi mzima.
Duru zadai jamaa alijaza mabango kwenye soko akitangaza huduma zake akidai alikuwa na ujuzi wa kuponya magonjwa yote na hata kutabiri nyota.
Alidai huduma zake zilikuwa bei nafuu na kutaka wenye shida kufika kwake au kupiga simu. Hata hivyo, hakuna mkazi aliyesaka huduma zake baada ya fununu kuenea kwamba jamaa alikuwa tapeli.
Baada ya kitumbua chake kuingia mchanga, jamaa huyo alifunga virago vyake na kuondoka.
**
KISAUNI, MOMBASA
Na JANET KAVUNGA
MWANADADA aliyekuwa akijigamba kwa kuweka kinyumba mume wa mtu alibaki kwenye mataa jamaa aliporudi kwa mkewe.
Mwanadada alikuwa akiwaambia wenzake kwamba hawajui mbinu za kunasa wanaume masonko na kuwafanya masponsa wao kwa kuwa jamaa alikuwa akitumia maelfu ya pesa kufadhili maisha yake ya anasa.
Wenzake walimuonya kwamba hafai kuringa na mume wa mtu lakini aliwapuuza akidai walikuwa wakimuonea wivu.
Juzi, jamaa aliondoka kwake na kumtumia ujumbe kumwarifu alikuwa amerudi kwa familia yake kisha akablock simu ya demu.
Kwa sasa, demu amekuwa akidandia tuktuk kwenda kazini ilhali jamaa alikuwa akimbeba kwa gari lake la kifahari kabla ya kumtema.
***
DARAJA MBILI, KISII
Na TOBBIE WEKESA
Kizaaza kilizuka katika baa moja ya eneo hili jamaa alipomlazimisha demu kuondoka. Inasemekana polo alimuamrisha kidosho amalizie chupa ya pombe aliyokuwa amemnunulia kisha waondoke.
“Malizia hiyo pombe tuondoke. Napigwa na baridi,” jamaa alimueleza kidosho. Duru zinasema kidosho alimueleza kwamba hakuwa tayari kuondoka kilabuni wakati huo.
“Dozi ndio sasa inabamba. Unataka niende kwa nyumba kufanya nini,” kidosho alifoka.
Penyenye zinasema jamaa alimkaribia kidosho na kumwaga pombe yote.
“Hii pombe ni mimi nimekununulia. Twende haraka. Siwezi kuendelea kupigwa na baridi hapa,” jamaa alimchemkia kidosho.
Inasemekana kidosho aliamua kuondoka kimyakimya bila kutazama nyuma.