MWANAUME ambaye alivuruga mkutano wa kisiasa wa Rais William Ruto katika eneo la Kondele, Kaunti ya Kisumu miaka miwili iliyopita, jana alitozwa faini ya Sh10,000 au akae jela kwa mwaka moja.
Wilson Aminda, aliadhibiwa kwa kuzua vurugu kwenye mkutano huo uliohutubiwa na Rais Ruto wakati huo akiwa Naibu Rais. Mahakama ya Winam ilimpata Aminda na hatia kwa kuharibu mali ya serikali na pia akatozwa faini nyingine ya Sh3,000 kwa kuzua fujo.
“Kwa makosa ya kwanza ya kuharibu mali ya serikali, mshtakiwa atalipa faini ya Sh10,000 au akae jela mwaka mmoja,” akasema Hakimu Mkuu Mkaazi wa Mahakama ya Winam Robert Oanda.
Hakimu huyo alisema ushahidi wote ulionyesha mshtakiwa alikuwa eneo la tukio. Bw Oanda alisema mshtakiwa angetumikia adhabu ya miaka mitano ila wale ambao walikuwa wanadai magari yao yalivunjwa, hawakuwasilisha malalamishi rasmi.
“Nimelinganisha ushahidi ambao ulionyeshwa na ni dhahiri kuwa mshtakiwa alikuwa eneo la tukio wakati wa ajali,” akaongeza.