NA LAWRENCE ONGARO
KAUNTI ya Kiambu inajenga ghala kubwa la kuhifadhi dawa zote za hospitali za kaunti hiyo.
Jumba hilo linajengwa katika Hospitali ya Ruiru Level 4 huku likitarajiwa kukamilika mwezi Machi 2023.
Gavana wa Kiambu Kimani Wamatangi alizuru hospitali ya Ruiru Level 4 ili kujionea mwenyewe mradi huo.
Alieleza kuwa hospitali hiyo ikikamilika itahifadhi dawa zote za hospitali katika kaunti yote huku ikitundikwa na mitambo ya kidijitali itakayofuatilia jinsi dawa zinavyotumika katika hospitali zote katika gatuzi.
Alisema tayari kaunti ya Kiambu imesambaza dawa katika hospitali zote ili kunufaisha wagonjwa wote wanaohudhuria hospitali za kaunti.
“Mhudumu yeyote atakayepatikana ameficha dawa za hospitali atachukuliwa hatua ya kisheria bila huruma,” alisema gavana huyo.
Ametoa onyo kwa wahudumu walio hospitalini kuhakikisha dawa zitakazohifadhiwa kwenye ghala hilo zinalindwa ili kunufaisha wagonjwa wote.
Aliwapa wakazi wa Kiambu nambari ya simu ya dharura iwapo mgonjwa atakosa dawa hospitalini afanye hima kwa kupiga nambari 0742000888.
Alisema atahakikisha wakazi wa Kiambu wanajisajili kuwa na Bima ya hospitali ya NHIF ili kuwarahisishia maswala ya afya.
“Sisi katika kaunti ya Kiambu tunataka wagonjwa kupata huduma ya maana bila kutumwa kununua dawa nje ya hospitali,” alifafanua gavana huyo.
Kaunti ndogo ya Ruiru imeongezeka kwa idadi ya wakazi ambapo wanakaribia milioni moja.