SHANGAZI,
Nimepata mwanamume mpenzi wa dhati aliye tayari kuwa mwenzangu maishani. Lakini kuna changamoto. Anasisitiza tupimwe lakini naogopa kwa sababu nimekuwa na wapenzi kadhaa ambao walichovya asali bila kinga. Nishauri.
Siku hizi hiyo imekuwa tahadhari ya lazima kwa wapenzi wanaothamini maisha yao. Hiyo ni fursa nzuri kwako kujua hali yako ya afya kwa manufaa yako na mpenzi wako. Ukikataa atakushuku na labda kubadili nia yake kuhusu uhusiano wenu.
Kuna mwanamke tuliyekutana juzi katika maskani ya starehe na tukapendana. Aliniomba pesa kushughulikia jambo la dharura na nikampa. Jana alinitumia ujumbe akaniambia nimkome eti ni mke wa mwenyewe. Nifanyeje?
Mwanamke huyo alitaka kukupora pesa tu na ndiyo maana alikubali ombi lako mara moja. Labda hata si mke wa mtu, hiyo ndiyo kazi yake. Usikate tamaa, hatimaye utapata mpenzi wa dhati.
Mpenzi wangu ana mimba yangu na nimeamua kumuoa. Lakini amekataa akisema anahitaji muda zaidi kufikiria. Simuelewi kwa sababu amekuwa akiniambia ananipenda.
Uamuzi wa mpenzi wako unatia shaka. Pendekezo la ndoa linafaa kutoka kwake kwa sababu anabeba mtoto wako. Kama anakupenda anataka kufikiria nini? Kuna uwezekano mkubwa kuwa hataki kuwa mke wako. Kuwa tayari kwa chochote kile.
Nina mpenzi na matumaini yangu ni kuwa hatimaye atakuwa mke wangu. Nimekuwa naye kwa miaka miwili sasa na nataka kuhakikisha ananipenda kwa dhati. Je, ninafaa kusubiri kwa muda gani?
Inaweza kuchukua miezi au miaka kadhaa kuthibitisha mapenzi ya dhati. Wapenzi wanapokubaliana kufunga ndoa huwa wamefikia kilele cha mapenzi yao na hatua hiyo ni thibitisho la mapenzi ya dhati.