Na SAMMY WAWERU
KIONGOZI wa chama cha Wiper Kalonzo Musyoka amesihi vinara wenza katika Okoa Kenya Alliance (OKA) kumpa tiketi ya muungano huo kupeperusha bendera ya urais uchaguzi mkuu ujao.
OKA inajumuisha Mabw Kalonzo, Musalia Mudavadi (ANC), Moses Wetangula (Ford-Kenya) na Gedion Moi (KANU).
Huku Bw Moi na ambaye ni seneta wa Baringo Alhamisi akitangaza azma yake kuwania urais 2022, Kalonzo amewahimiza vinara wenza katika OKA kumpa tiketi ya urais akihoji yeye ndiye tiba ya changamoto zinazozingira Wakenya.
“Muniombee niteuliwe kupeperusha bendera ya OKA kugombea urais. Nikiteuliwa tutafanya kazi pamoja na ndugu yangu Gedion Moi,” Bw Kalonzo akasema, akizungumza katika kongamano la KANU, Ukumbi wa Bomas, jijini Nairobi.
“Haya mambo mtuachie, mimi na Gedion,” kiongozi huyo wa Wiper akaonekana kurai vinara wenza katika OKA, akielezea uhusiano wake wa karibu na Rais (mstaafu) Daniel Arap Moi ambaye kwa sasa ni marehemu.
Mabw Raila Odinga (ODM), Mudavadi, Wetangula, na Isaack Ruto (Chama Cha Mashinani) ni kati ya wageni mashuhuri waliohudhuria hafla hiyo ya KANU. Raila na Mudavadi pia wameashiria kugombea urais 2022, kumrithi Rais Uhuru Kenyatta.
Naibu wa Rais Dkt William Ruto anaendeleza kampeni kusaka kura kuwa rais wa tano wa Jamhuri ya Kenya.