• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 4:42 PM
Kaunti za Pwani kusaka ?watalii kama eneo moja

Kaunti za Pwani kusaka ?watalii kama eneo moja

Na SIAGO CECE

SERIKALI ya Kaunti ya Mombasa itashirikiana na kaunti zingine za Pwani kuinua sekta ya utalii ambayo imepata pigo kubwa katika miaka ya hivi majuzi.

Kupitia mpango wa ‘Sister Cities’ ambao hulenga kutafuta ushirikiano wa miji ya kimataifa kuvutia utalii, kaunti hiyo ikiongozwa na Gavana Hassan Joho imeanza kutafuta umoja wa Pwani kitalii, ikianza na Kaunti ya Kwale.

Akizungumza katika Hoteli ya Neptune Beach iliyo Diani, Kaunti ya Kwale, Afisa Mkuu wa Vijana, Jinsia na Michezo katika Kaunti ya Mombasa, Bw Innocent Mugabe alisema mpango huo unakusudia kukuza utalii katika eneo lote la Pwani na kuvutia watalii zaidi wa kimataifa ambao idadi yao imepungua kwa sababu ya janga la corona.“Kaunti ya Kwale ni ya kipekee.

Hatuangalii tu Kaunti ya Mombasa, lakini pia kaunti nyingine jirani kwa sababu hatuwezi kuuza Pwani ya Kenya kupitia kwa kaunti moja tu,” Bw Mugabe alisema.

Alikuwa akizungumza alipoandamana na waandishi wa habari na maajenti wa utalii na usafiri kutoka Ukraine waliotembelea Kwale, ili kugundua vivutio ambavyo vinaweza kuwafuraisha watalii wa Kiukreni.

Kaunti ya Mombasa ilitia saini ushirika wa utalii na serikali ya Ukraine kufufua sekta ya utalii kupitia mpango maalumu wa ‘Sister Cities’.

Bw Mugabe aliongeza kuwa Kaunti za Taita Taveta na Kilifi pia zinalengwa kutokana na vivutio kama vile Mbuga ya Wanyama ya Tsavo ambayo inajulikana kwa wanyama pori na uhamiaji wa nyangumi huko Watamu, Kilifi, ambao kwa muda mrefu umevutia watalii kutoka kote ulimwenguni.

Balozi wa Ukraine nchini, Bw Oleksii Sierkov alisema kuwa tayari, ndege zaidi za kukodisha zimepangwa kuleta watalii kutoka nchi yake ambao watatua kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Moi, Mombasa.Wiki hii, watalii zaidi ya 200 wanatarajiwa kuwasili Mombasa.

‘Tangu tuanze ushirikiano huu, zaidi ya watalii 1,000 kutoka Ukraine wamefika Kenya na tunatumaini pia kwamba Wakenya wengi watatembelea Ukraine,’ alisema balozi huyo katika mahojiano akiwa Kaunti ya Kwale.

Mkurugenzi wa mpango huo wa Sister City, Bi Salma Noor alisema angalau miji 22 ya kimataifa imekubali kushirikiana na Kenya kupitia mpango huo wakati miji kutoka Ukraine tayari imeahidi kuwa na ndege zao za kukodi kwenda Mombasa.

‘Miji mingine mingi sasa inavutiwa kujisajili nasi na hii itaongeza idadi ya watalii huko Mombasa ambao pia watatembelea kaunti nyingine,’ alisema, akisisitiza kuwa lengo ni kunufaisha kaunti zote katika eneo la Pwani.

Hivi sasa, utalii wa kimataifa umeanza kuimarika Pwani na hoteli nyingi zinarekodi idadi kubwa za watalii kutoka nchi za nje ikilinganishwa na mwaka jana.

You can share this post!

Nilitarajia Messi atoe ombi la kuchezea Barcelona bila...

Wetang’ula apuuza Eseli mzozo ukitokota Ford- Kenya