NA BRIAN OCHARO
MAHAKAMA ya Mombasa imewataka maafisa wawili wakuu wa polisi waliochunguza kesi dhidi ya Bw Elsek Osman, raia wa Uturuki aliyeshtakiwa kwa madai ya unajisi na ukahaba wa watoto kufika mbele yake.
Hii ni baada ya ripoti ya polisi kudai kuwa, kesi hiyo ilianzishwa kwa nia mbaya iliyokiuka sheria.
Hati zilizowasilishwa katika Mahakama Kuu ya Malindi pamoja na mahakama za Kilifi na Mombasa zimedai ushahidi uliotumiwa mahakamani ulibuniwa.
Hakimu Mwandamizi Vincent Adet, amewataka maafisa hao wafike mahakamani ili wajieleze kwa nini mshukiwa hajapewa taarifa za baadhi ya mashahidi wakuu ili kesi hiyo ianze kusikizwa.
Amri hiyo ilitolewa baada ya kiongozi wa mashtaka, Bw Hillary Isiaho, kusema maafisa hao walipewa hati ya kuwaitwa mahakamani lakini wakapuuza.