• Nairobi
  • Last Updated May 10th, 2024 4:39 PM
Msako wa walioua kinyama Kaniss na Omodollar na kuweka nyama zao kwenye gunia waendelezwa 

Msako wa walioua kinyama Kaniss na Omodollar na kuweka nyama zao kwenye gunia waendelezwa 

NA MWANGI MUIRURI
WAPELELEZI katika Kaunti za Nairobi na Machakos wanaendeleza msako dhidi ya walioua musoshiolaiti Rachel Kanini almaarufu Kaniss na mpenzi wake aliyejulikana kama Omodollar na kisha kupakia nyama zao ndani ya gunia.

Omodollar anaripotiwa kuwa raia wa Nigeria na haieleweki biashara aliyokuwa akivurumisha hapa nchini, licha ya kuonekana akiishi maisha ya kifahari akiwa na mrembo wake Kaniss.

Ripoti ya uchunguzi inaonyesha kwamba kinachochunguzwa kwa sasa ni nia ya mauaji hayo ya kikatili yaliyoanza na kutekwa nyara kwao mnamo Juni 25, 2023.

Miili yao ilipatikana Alhamisi wiki iliyopita, saa za jioni ikiwa imekatakatwa vipandevipande na kisha kupakiwa kwenye gunia na kufichwa katika kichaka cha Nguluni Kaunti ya Machakos.

Ajabu ni kwamba, walitupwa karibu na nyumba ya wazazi wa Bi Kanini na polisi wamesema wanachunguza uwezekano wa uhasama wa kibiashara, uhusiano na mtandao wa ujambazi, kisasi cha kimapenzi, urushanaji katika dili au ukora wa kawaida katika mauaji hayo.

Ripoti ya maafisa wa polisi waliofika kuchukua mabaki hayo huku wakizindua uchunguzi walisema kuwa hicho ni kisa wazi cha mauaji.

“Miili ya wawili hao ni kisa cha ujambazi wa utekaji nyara na kisha mauaji ya kikatili. Uchunguzi umezinduliwa,” ripoti hiyo ya kitengo cha uchunguzi wa uhalifu wa jinai (DCI) waonyesha.

Kitengo hicho kilisema kwamba eneo walipopatikana limedhibitiwa, na uchunguzi wa kimaabara umezinduliwa huku waliokuwa wa mwisho kuonekana nao na pia kuzungumza nao kwa njia za aina zozote zile za mawasiliano wakiombwa kujitokeza kuandikisha taarifa.

Ripoti ya upasuaji wa miili hiyo inatarajiwa kuongeza makali ya uchunguzi kwa kubainisha njia halisi iliyotumika kutekeleza ukatili huo.

[email protected]

 

  • Tags

You can share this post!

Seneta Methu: Wanaopinga Mswada wa Fedha 2023 ni sawa na...

Rapudo amnunulia mkewe Amber Ray ‘nywele’ za...

T L