CHAMA cha ODM kimekashifu wapinzani wake wanaodai kimepoteza umaarufu eneo la Pwani baada ya wanachama wengi kuamua hawatakitumia kuwania viti vya kisiasa ifikapo mwaka wa 2022.
Gavana wa Mombasa, Bw Hassan Joho alisisitiza Jumamosi kwamba chama bado kiko imara Pwani akapuuzilia mbali madai kuwa kimekuwa dhaifu.“Wanasema ODM Pwani imelegea. Mimi nasema ODM bado ni maarufu,” akasema.
Maoni haya yaliungwa mkono na aliyekuwa diwani wa Mkongani, Kaunti ya Kwale, Bw Hassan Chitembe ambaye alisema Bw Odinga bado ana ufuasi mkubwa eneo hilo.Kulingana naye, ubinafsi wa viongozi wa Pwani ndio umewafanya baadhi yao kuanza kuzungumzia kuunda vyama vipya huku wengine wakihamia mrengo wa Naibu Rais William Ruto ulio maarufu kama Tangatanga.
“Viongozi wengi hawa kama si Baba (Raila) hawangekuwa mamlakani. Wamefanya kubebwa na mzee na sasa ndio wanatangatanga wakimtusi,” akasema Bw Chitembe ambaye ni mmoja wa wafuasi wakuu wa ODM eneo hilo.
Hivi majuzi, Mbunge wa Magarini Michael Kingi alijiunga kwenye orodha hiyo ya viongozi wanaopanga kuutumia vyama vingine 2022.Mbunge huyo alitangaza kuwa chama atakachotumia ni kile ambacho kitaundwa baada ya mashauriano ya baadhi ya viongozi wanaotaka kuwe na chama mahususi cha Pwani.
Mashauriano hayo yanaongozwa na Gavana wa Kilifi, Bw Amason Kingi ambaye ndiye mwenyekiti wa ODM katika kaunti hiyo kwa sasa.“Nilichaguliwa kupitia ODM na ninasema hapa wazi kwamba ifikapo 2022, nitakuwa nimeondoka katika chama hicho.
Wale wanaotaka kuendelea kukiunga mkono chama hicho waendelee lakini kwangu mimi, nitakuwa katika chama cha eneo langu,” akasema.Mbunge huyo ni miongoni mwa wanasiasa wanaolenga kurithi kiti cha ugavana Kilifi.Katika Uchaguzi Mkuu wa 2017, Kaunti ya Kilifi ilikuwa na ufuasi mkubwa wa ODM kiasi cha kwamba wabunge wote saba, mbunge mwakilishi wa wanawake, seneta na gavana ni wanachama wa chama hicho kinachoongozwa na Bw Raila Odinga.
Wao ni wabunge Owen Baya (Kilifi Kaskazini), Ken Chonga (Kilifi Kusini), William Kamoti (Rabai), Paul Katana (Kaloleni), Michael Kingi (Magarini), na Aisha Jumwa (Malindi), kando na mbunge mwakilishi wa wanawake Getrude Mbeyu na Seneta Stewart Madzayo.
Mbali na hayo, madiwani 27 kati ya 35 waliochaguliwa Kilifi ni wanachama wa ODM. Hivi majuzi madiwani hao walikutana na Bi Jumwa, na kuashiria uwezekano wao kuanza kuegemea upande wa Naibu Rais William Ruto.
Kufikia sasa, Bw Mwambire, Bw Chonga, Bi Mbeyu na Bw Madzayo pekee ndio wameonekana kuendelea kuwa waaminifu kwa chama.Katika Kaunti ya Kwale, ODM ilipoteza moja ya viti vyake viwili vya ubunge eneobunge la Msambweni baada ya kifo cha aliyekuwa mbunge Suleiman Dori. Kabla kufariki kwake, alikuwa tayari ashaanza kuzozana na chama hicho.
Uchaguzi mdogo ulishindwa na Bw Feisal Bader aliyewania bila kutumia chama ingawa aliungwa mkono na viongozi wanaoegemea upande wa Dkt Ruto.Mbunge aliyebaki wa ODM kaunti hiyo ni wa Kinango, Bw Benjamin Tayari.Gavana wa kaunti hiyo, Bw Salim Mvurya alihama ODM akatumia Chama cha Jubilee kuwania ugavana 2017. Hii ilikuwa ni baada ya mizozo kuibuka kati yake na Gavana Joho.