Na GEOFFREY ANENE
MACRINE Kalombo alishindia Kenya medali yake ya kwanza ya dhahabu kwenye mashindano ya kuogelea ya Afrika ya Zoni ya Nne yaliyoingia siku ya pili jijini Lusaka, Zambia, hapo Ijumaa.
Kalombo alitwaa taji la kuogelea mita 200 (Breaststroke) kwa washiriki walio na umri wa miaka 12 ama chini. Alitumia dakika 3:12.27 akifuatiwa kwa karibu na Mkenya mwenzake Christie Kamotho (3:15.25) na mwenyeji Adrianna Bhana (3:18.60).
Kufikia Ijumaa jioni, Wakenya walikuwa wamezoa jumla ya medali nane (dhahabu moja, fedha tano, shaba mbili). Medali ya Kamotho ilikuwa yake ya pili baada pia kunyakua fedha katika kuogelea mita 50 (Breaststroke). Duini Caffini ana nishani za fedha za mita 50 na mita 200 (Breaststroke) katika kitengo cha waogeleaji walio kati ya umri wa miaka 13 na 14.
Maria Bianchi aliridhika na medali ya shaba kuogelea mita 800 (Freestyle) kwa washiriki walio na umri wa kati ya miaka 15 na 24 naye Ameya Rana akawa nambari sita. Imara-Bella Thorpe alipata nishani ya fedha katika kuogelea mita 100 (Backstroke) kwa waogeleaji walio na umri wa miaka 17 hadi 29. Nathan Matimu alikuwa ameshindia Kenya medali ya pekee ya wavulana aliporidhika na shaba ya mita 800 (Freestyle) kwa washiriki walio na umri wa miaka 14 ama chini.