NA SAMMY WAWERU
RAIS William Ruto ameliongoza taifa kumuomboleza mtangazaji maarufu wa miaka mingi, Bi Catherine Kasavuli aliyefariki kutokana na ugonjwa hatari wa saratani.
Bi Kasavuli ameugua kwa muda mrefu saratani ya mlango wa uzazi na habari za kifo chake Alhamisi usiku zilitolewa na Mkurugenzi Mkuu Shirika la Habari la Kenya (KBC), Bw Samuel Maina.
Hadi kufariki kwake, mwanahabari huyo alikuwa mfanyakazi wa shirika hilo la serikali ambapo alikuwa akiendesha shoo ya Legend Edition kila wikendi.
Dkt Ruto alimtaja marehemu kama mtangazaji mchangamfu na mkakamavu kwenye utendakazi wa kipekee.
“Alikuwa mtangazaji machachari aliyepamba runinga zetu,” Rais ameomboleza.
Bi Kasavuli alijiunga na tasnia ya uanahabari mwaka wa 1980 akiwa na umri wa miaka 22, katika shirika la Voice of Kenya (VoK) ambalo kwa sasa linaitwa KBC.
Mama wa Taifa, Bi Rachael Ruto amesema marehemu alikuwa mwanamke mwenye malengo na maono makuu, akiongozwa na nidhamu kwenye utendakazi wake.
“Hata ikiwa hukufurahia habari, ungeridhishwa na jinsi alivyopeperusha na kusalia ukitazama runinga,” Bi Ruto akamkumbuka.
Naye Waziri wa Ulinzi, Bw Aden Duale amemtaja mwendazake kama mwanahabari aliyepamba runinga kwa madaha kutokana na ufasaha wake.
Waziri wa Michezo, Ababu Namwamba amemuomboleza Kasavuli kama kielelezo kutokana na jitihada zake kukuza vipaji katika uanahabari.
“Nilikuwa nikivutiwa na ustadi, urembo na ujuzi unaposoma habari. Hatimaye, ulinishawishi nikakuiga na kujiunga na uanahabari,” Naisula Lesuuda, mbunge wa sasa Samburu Magharibi aliandika kwenye Twitter.
Mbunge huyo aliwahi kuhudumu kama mtangazaji KBC, kabla kujiunga na siasa.
Kasavuli alifariki katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta (KNH) alipokuwa akipata matibabu akiwa na umri wa miaka 60.
Subscribe our newsletter to stay updated