NA CHARLES WASONGA
SERIKALI ya Kenya imekana habari zilizosambazwa na shirika la habari la Reuters kwamba wadukuzi wa mitandao kutoka China walishambulia wavuti na kanzidata za Ikulu, wizara na idara nyingine za serikali.
Katibu katika Wizara ya Usalama Raymond Omollo, kwenye taarifa aliyoituma kwa vyombo vya habari Alhamisi jioni, alielezea ripoti hiyo iliyosambazwa Jumatano kama “propanda isiyo na msingi wowote.”
“Makala hayo yachukuliwe kama propaganda iliyodhaminiwa. Usambazaji wa habari hizi na mashirika mengine ya kigeni ya habari unaashiria njama yao kuingilia uhuru wa Kenya,” Dkt Omollo akasema.
Taarifa hiyo ya serikali ya Kenya inajiri baada ya Ubalozi wa China kutoa taarifa nyingine sawa na hiyo ikipuuzilia mbali ripoti hizo.
Ubalozi huo ulitaja ripoti hizo kama “zisizo na msingi, uvumi na zisizo na maana yoyote.”