NA FARHIYA HUSSEIN
WADAU katika sekta ya utalii wamemrai Rais Uhuru Kenyatta kushughulikia changamoto zinazowakumba kabla aondoke mamlakani.
Wakieleza lalama zao baada ya mashirika ya ndege ya Uturuki kusitisha safari za Mombasa, walisema sekta hiyo inazidi kusahaulika serikalini.
Shirika la Ndege la Uturuki lilitoa taarifa kwa wateja wake kwamba, safari za ndege ambazo zilitarajiwa kufanyika kuelekea Mombasa mwaka huu zilisitishwa hadi Oktoba.
Aliyekuwa Mwenyekiti wa Shirikisho la Utalii la Kenya, Bw Mohammed Hersi alimtaka Rais atoe amri kuruhusu mashirika ya ndege ambayo yanataka kusafiri moja kwa moja hadi Mombasa yawe huru kufanya hivyo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wafanyabiashara wa Hoteli na Wafanyabiashara wa Pwani, Dkt Sam Ikwaye, alilalamika kuwa wadau wa utalii walisahaulika chini ya uongozi wa Rais Kenyatta.