NA GEORGE ODIWUOR
GAVANA wa Homa Bay Gladys Wanga anayataka mashirika yanayohusika na usalama wake kueleza ni kwa nini mlinzi wake aliondolewa wiki jana.
Gavana huyo ambaye ni miongoni mwa kundi la wanasiasa wanaoegemea muungano wa Azimio La Umoja – One Kenya Raila Odinga alisema hahisi salama baada ya mlinzi wake kuondolewa na serikali kwa sababu ambazo hakulezewa.
Bi Wanga, pamoja na Magavana wengine wa Nyanza Anyang Nyong’o (Kisumu), James Orengo (Siaya) na Ochilo Ayacko (Migori) walipokonywa walinzi wao wiki jana.
Hii ni baada ya kinara wa Azimio, Bw Raila Odinga kuitisha maandamano kuishinikiza serikali kupunguza gharama ya bidhaa za kimsingi.
Bi Wanga alisema kufikia sasa, hakuna maelezo yoyote ambayo yametolewa kwake kuhusu ni kwa nini mlinzi wake aliondolewa.