NA JAMES MURIMI
ASKOFU Mkuu Anthony Muheria wa Dayosisi ya Nyeri ya Kanisa Katoliki amekosoa serikali kwa kuendelea kuongeza ushuru na bei za mafuta akisema zinawalemea Wakenya na kuwafanya masikini zaidi.
Askofu Muheria anataka serikali kuzungumza na viongozi wa kidini na wadau wengine ili kuwakinga raia na athari za ongezeko la bei zinazowaumiza.
“Tunahitaji mdahalo kuhusu iwapo hivi ndivyo tunapaswa kufanya, hasa katika hali hii ambayo bei za mafuta zimeongezeka kwa kiwango kikubwa. Kwa hakika tunasakama Wakenya na masikini ndio watateseka. Tunahitaji kuungana na serikali na wadau wengine ili kutafuta suluhu la kudumu kuhusu suala hili kwa kuzuia ongezeko hili,” alisema Askofu Muheria akihutubia wanahabari katika Our Lady of Consolata Cathedral mjini Nyeri.
Alilaumu viongozi kwa kutoweka mbele maslahi ya Wakenya na kuongeza kuwa wamekuwa wakifanya hivyo kwa mdomo lakini vitendo vyao ni tofauti.
“Wale wanaoumia wataendelea kuumia zaidi. Kwa mfano bei ya mafuta taa imeongezeka kwa Sh33. Kusema kweli ni masikini watakaoumia zaidi,” alisema.
Lakini waziri wa Uchukuzi Bw Kipchumba Murkomen alitetea serikali akisema bei za mafuta zimeongezeka kote ulimwenguni.