NA CHARLES WASONGA
MAGARI yamekuwa machache zaidi katikati mwa jiji la Nairobi leo Jumatano asubuhi kufuatia taharuki iliyochangiwa na maandamano yaliyoitishwa na muungano wa Azimio La Umoja-One Kenya na mgomo wa madereva wa magari.
Kufikia mwendo wa moja na nusu asubuhi, barabara za Moi Avenue, Kimathi Street, na barabara ya Koinange miongoni mwa nyingine zimekuwa na idadi ndogo zaidi ya magari.
Hata hivyo, kumekuwa na magari machache ya matatu katika baadhi ya vituo vya matatu Khoja, Tea Room, OTC barabara ya Tom Mboya na Ronald Ngala.
Polisi walionekana wakishika doria katika baadhi ya barabara kadhaa za Nairobi wakilinda doria kuhakikisha kuwa waandamanaji hawafiki hawaingii katikati mwa jiji.
Maduka mengi yalikuwa yamefungwa majira ya asubuhi, wenyewe wakihofia hasara kutokana na makabiliano kati ya polisi na waandamanaji.
Duru zimesema kuwa baadhi ya wanafunzi hawakuenda shuleni baada ya wasimamizi wa shule hizo kuwashauri wasalie nyumbani.
Kamanda wa polisi katika Kaunti ya Nairobi Adamson Bungei alisema hawataruhusu mikutano yoyote katikati na viungani mwa jiji la Nairobi.
“Hakutakuwa na mkutano wowote Kamukunji au mahala popote jijini. Tumewaambia waandalizi kwamba mkutano wao hautakuwepo jijini Nairobi,” Bungei akasema akiongeza kuwa polisi wa kutosha wameletwa jijini kudumisha amani.
Mnamo Jumanne, Inspekta Jenerali wa Polisi Japhet Koome alipiga marufuku maandamano yaliyopangwa na Azimio katikati mwa jiji na maeneo mengine nchini.