• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 9:35 PM
Urusi yaua watu 14 mjini Zaporizhzhia

Urusi yaua watu 14 mjini Zaporizhzhia

Na AFP

ZAPORIZHZHIA, UKRAINE

WATU 14 wameuawa katika shambulio la makombora lililotekelezwa na Urusi katika mji wa Zaporizhzhia kusini mwa Ukraine, utawala wa mji huo umetangaza.

Makombora hayo yalianguka katikati mwa mji huo, umbali wa kilomita 40 kutoka eneo la kusini mwa mji huo ambako mapigano yalichacha juzi.

“Tumepata habari ya kuhuzunisha baada ya kukagua jengo lililopigwa wakati wa shambulio hilo,” akasema katibu wa baraza la mji huo Anatoly Kurtev.

“Kufikia sasa idadi ya waliokufa imepanda hadi kufika 14,” akaongeza.

Ripoti za mwanzo kuhusu mashambulio hayo ya makombora zilisema kuwa mtu mmoja aliuawa na wengine saba wakajeruhiwa.

Lakini baadaye shirika la kushughilikia mikasa lilisema idadi ya waliokufa ilipanda hadi kufikia 11.

Jengo la makazi lenye orofa tano, lililoko kando ya barabara kuu mjini humo liliporomoka kabisa katika shambulio hilo.

Rais Volodymyr Zelensky amelaani shambulio hilo akilitaja kama “uhalifu uliotekelezwa kimakusudi”.

“Haikubaliki kwamba mji wa Zaporizhzhia hushambuliwa kwa roketi na makombora kila siku. Huu ni uhalifu wa kimakusudi,” Zelensky akasema kwenye taarifa aliyotoa Jumamosi kupitia video.

Japo mji huo wa kiviwanda unadhibitiwa na serikali ya Ukraine, kiwanda cha kinyuklia kilichoko humo kimedhibitiwa na wanajeshi wa Urusi.

Hata hivyo, Urusi inadai kudhibiti eneo zima la Zaporizhzhia lakini wanajeshi wake hawajafaulu kuteka maeneo kadha.

Serikali ya Ukraine inasema watu 30 waliuawa wiki jana katika kisa ambapo msafara wa magari ya kibinafsi yalishambuliwa.

Ilidai kuwa shambulio hilo lilitekelezwa na wanajeshi wa Urusi, ingawa uongozi wa Urusi umekana madai hayo.

Wakati huo huo, daraja muhimu linalounganisha Urusi na eneo la Crimean jana liliporomoka baada ya gari moja kulipuka.
Daraja hilo ndilo hutumika na Urusi kupitisha vyakula na mahitaji mengine kwa wanajeshi wake wanaendeleza mapigano nchini Ukraine.

Baada ya tukio hilo katika daraja hilo kwa jina Kerch, maafisa wa Ukraine walituma jumbe kupitia mitandao ya kijamii walielezea kufurahishwa na mkasa huo.

Urusi ilitwaa eneo la Crimea kutoka kwa Ukraine mnamo 2014. Baadaye daraja hilo kubwa na lenye urefu wa kilomita 19 lilifunguliwa rasmi miaka minne baadaye na Rais wa Urusi Vladimir Putin, mwenyewe.

Bado haijabainika ikiwa mlipuko huo ulikuwa ni shambulio la kimakusudi au la. Lakini maswali yameibuliwa kuhusu kuharibiwa kwa muundo msingi mkubwa kama huo wakati ambapo wanajeshi wa Urais wameonekana kupoteza maeneo kadhaa kwa wanajeshi wa Ukraine.

  • Tags

You can share this post!

Muhoozi: Ruto katika njia panda

Uchaguzi wa Agosti 9 ulilenga kutimua waenezaji wa chuki za...

T L