NA WANGU KANURI
WATAALAMU wa afya wameonya dhidi ya matumizi ya simu mtu aendapo msalani. Kuketi msalani kwa muda mrefu pamoja na kukaza haja kunahatarisha sehemu zako nyeti kuugua ugonjwa wa bawasiri (hemorrhoids).
Ugonjwa huu hufanya mishipa ya damu iliyochomoza katika sehemu ya rektamu na tupu ya nyuma kufura huku mgonjwa akipata maumivu na hata kutokwa na damu.
Hata ingawa mtu hakazi haja, kuchuchumaa kwenye kiti cha choo hutia presha kwenye mishipa ya sehemu nyeti na kufanya haja ikose kutoka ipasavyo hivi kufanya choo kiwe kigumu na akatatizika anapoenda haja kubwa.
Hata hivyo, ili kuepukana na ugonjwa huu, ni vyema kupungiza muda unaotumia uendapo haja kubwa na hata kukanyaga stuli.
Hii ni kwa sababu unapoinua miguu yako, unaweza kuenda haja kwa urahisi. Pia ni muhimu kubadilisha chakula chako ukala matunda mengi kama tufaha, kiwi, mapera, na mengine yenye vitamini C pamoja na kunywa maji mengi.
Kuenda na simu msalani pia kunahatarisha uwezekano wa bakteria kuenea nje ya choo na hata nyumba nzima na kusababisha magonjwa.
***
Shirika la Afya Duniani (WHO), kwa ushirikiano na Age and Ageing, jarida la Chama cha Wazee wa Uingereza (British Geriatrics Society), lilizindua toleo maalum kuhusu vipimo vya kuangazia afya ya wazee ya akili, mwili na wanavyoshirikiana na jamii kwa ujumla.
Ifikapo mwaka wa 2030, mtu mmoja kwa wengine sita duniani watakuwa na umri wa miaka 60.
Wakati huo, watu wazee watakuwa wameongezeka kwa bilioni 1.4 kutoka bilioni 1 tangu mwaka wa 2020.
Idadi hii itakuwa maradufu ifikapo mwaka wa 2050 (wazee watakuwa bilioni 2.1).
Watu walio na umri wa miaka 80 na zaidi watakuwa wameongezeka mara tatu kutoka mwaka wa 2020 hadi 2025 na wakafika milioni 426.
Huku idadi ya wazee ikiongezeka, WHO inasema kuwa mazingira yao hayajaimarishwa huku wengi wakiwa kwenye hatari ya kuwa na afya duni na hata ulemavu.
Kwa kuelewa wanachohitaji wazee hawa, WHO inaeleza kuwa jamii zitaweza kuwapa heshima watu wanaozeeka.