• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 11:33 PM
Ninaenda ‘break’ mashabiki mnisubiri – Akothee

Ninaenda ‘break’ mashabiki mnisubiri – Akothee

NA FRIDAH OKACHI

MFANYABIASHARA na mwanamuziki Esther Akoth almaarufu ‘Akothee’, alitangaza atachukua mapumziko kwenye mitandao ya kijamii kutokana na kufanya kazi bila mapumziko, jambo linalomsababishia uchovu na mwili kunyong’onyea.

Kwenye posti ndefu kupitia kurasa za akaunti zake za mitandao ya kijamii ya Facebook na Instagram, mama huyo wa watoto watano alisema atakosekana kwenye mitandao yote ya kijamii hadi katikati mwa Januari 2024.

Alisema matukio ya 2023 yamemfanya achoke sana na hivyo anahitaji kupumzika kwa muda ili kurejesha nguvu.

“Wapendwa mashabiki, natumai ujumbe huu utawapata mkiwa sawa… Mwaka huu unaokamilika umekuwa ni safari ya ajabu iliyojaa pandashuka. Ninamshukuru kila mmojawapo wa mashabiki kwa kuwa sehemu ya safari hii,” alisema Akothee.

Akaongeza: “Hata hivyo, jinsi safari ya maisha inavyozidi kuwa mbaya, ninajikuta nikihisi uchovu na kukosa nguvu. Msongamano wa mara kwa mara umeniacha nikiwa na wakati mchache wa kupumzika na kuongeza nguvu, na nimefikia hatua ambayo ninahitaji kutanguliza ustawi wangu.”

Msanii huyo mwenye umri wa miaka 43 alisema mapumziko hayo, yatamruhusu kujiongezea nguvu na pia kujiratibu upya.

Hatua hiyo ikiwa ni muhimu kuhakikisha kwamba anaweza kuendelea kutoa yaliyo bora kwa mashabiki wake.

Pia, aliwashukuru wale wote ambao walitoa msaada mwaka mzima.

“Ninaelewa umuhimu wa kuwepo kikamilifu na kutoa vitu bora zaidi na sitaki kuathiri ubora na uzoefu ninaoshiriki nanyi. Ninaamini kwamba mtaheshimu hitaji langu la mapumziko. Ninatazamia kuungana nanyi nyote katika mwaka mpya, tukiwa tumeburudishwa na tayari kwa matukio mapya,” alisema Akothee.

Mwanamziki huyo amekuwa gumzo mitandaoni mwaka 2023 baada ya kufunga ndoa, kisha akachukua talaka na pia kuhitimu na hivyo kutunukwa shahada ya digrii baada ya kusoma kwa takriban miaka 10.

  • Tags

You can share this post!

‘Tunataka stima madhubuti 2024’

Buda Murang’a alivyosherehekea Krismasi kwa bajeti ya...

T L