NA CHRIS ADUNGO
JAPO Laura Nyamvula Rua ni mwanahabari kitaaluma, kinachompa riziki ya kila siku kwa sasa ni fani ya uanamitindo, fasheni na ulimbwende pamoja na sanaa ya uigizaji ambayo imempa fursa ya kuvalia kofia tele katika ulingo wa filamu.
Kubwa zaidi katika maazimio yake ni kuwa miongoni mwa wasanii watakaotikisa ulimwengu wa uigizaji kwa kushiriki na kufyatua michezo ya runingani itakayokubalika zaidi kimataifa.
Analenga pia kupanua wigo wake wa ujasiriamali, kuwa mwanadiplomasia na kurejea katika tasnia ya uanahabari huku akilea na kukuza vipaji vya waigizaji chipukizi katika ngazi na viwango tofauti.
Baada ya kukamilisha mtihani wa KCSE mnamo 2014, Laura alihiari kusomea uanahabari japo matamanio yake yalikuwa kuwa mhudumu wa ndege (Cabin Crew Air Hostess).
Alishiriki mafunzo ya nyanjani katika Raia TV jijini Mombasa mnamo 2018 na akaajiriwa baadaye kuwa ripota na mhariri katika runinga hiyo hadi mwaka wa 2020.
Kipawa cha uigizaji kilimteka baada ya muda mfupi na akashiriki filamu ‘Acting Ndio Action’ iliyofyatuliwa na Maisha Magic East – DStv mnamo Machi 2022. Awali, alikuwa amenogesha filamu ‘Mizizi’ iliyompa jukwaa la kudhihirisha ukubwa wa uwezo wake katika uigizaji.
Laura alikulia na kulelewa katika mtaa wa Kiembeni ulioko eneo la Bamburi, Kaunti ya Mombasa. Ndiye kitinda mimba katika familia ya watoto watano wa Bw Michael Jefwa Rua na Bi Sheilla Ngulwa.
Alianza safari ya elimu katika shule ya msingi ya St Augustine’s Preparatory Tudor jijini Mombasa kabla ya kujiunga na shule ya upili ya Coast Girls (2010-2012) kisha Presbyterian High iliyoko Mariakani, Mombasa (2013-2014).
Alisomea stashahada (diploma) ya uanahabari na mawasiliano ya umma katika Chuo cha Kiufundi cha Mombasa (TUM) kati ya 2016 na 2019. Amekuwa mwanafunzi wa shahada ya kwanza katika masuala ya uanadiplomasia katika Chuo Kikuu cha Kenya Methodist (KeMU) tangu mwaka wa 2020.
Akiwa mwanafunzi wa sekondari, Laura alikuwa mwanachama wa Chama cha Uanahabari. Nafasi hiyo ilimpa majukwaa tele ya kuzungumza mbele ya hadhira, akanoa kipaji cha ulumbi na kuinua kiwango chake cha umilisi wa lugha.
“Kuhutubia wanafunzi na kusoma habari za matukio mbalimbali gwarideni kulinishajiisha sana,” anakiri.
Kwa mtazamo wake, uigizaji ni jukwaa linalozidi kutoa fursa za kuthaminiwa kwa tamaduni za jamii mbalimbali, kupitisha elimu, kukuza maadili, kubainisha taratibu za maisha na kuchangia ubidhaaishaji wa lugha.
“Kufaulu katika fani ya filamu na tasnia ya uanahabari ni zao la imani, bidii, stahamala na nidhamu. Usiogope kujaribu,” anashauri.
Anashikilia kuwa maigizo mazuri yanastahili kufumbata ubunifu na kusawiri uhalisia wa maisha. Aidha, mwigizaji bora lazima awe mfaraguzi, mwepesi wa kusoma hadhira na mjuzi wa kusuka na kusana maneno.
“Mwigizaji asiye na ujuzi wa kutumia lugha kwa ufundi hukosa uhuru wa kusema anachokitaka kwa jinsi anavyotamani kifikie hadhira. Ingawa uhuru wa mwigizaji umo katika utashi na falsafa, lugha ndicho kitovu cha maigizo na kamba inayovuta hadhira kwa dhamira ya sanaa yenyewe,” anasema.
Subscribe our newsletter to stay updated